Hospitali katika ukanda wa Gaza zinakabiliwa na upungufu wa vifaa vya matibabu kuokoa wahasiriwa waliojeruhiwa vibaya. / Picha: Reuters

Jumamosi, Oktoba 21, 2023

13:00 GMT - Israeli inataka watu wote wakiwemo wagonjwa waondoke kutoka hospitali 20 kaskazini mwa Gaza, kwa mujibu wa afisa mmoja wa usalama wa Israel.

"Hospitali nne zilikataa maagizo ya kuhama huku zingine zikiwa katika harakati za kuhamishwa," afisa huyo ambaye hakutajwa jina aliambia Shirika la Utangazaji la Israel.

Afisa huyo alidai kuwa "Wapalestina wapatao 30,000 walikuja kwenye makao yanayozunguka Hospitali ya Shifa kutumika kama ngao za binadamu."

12:000 GMT - Mafuta hayataletwa Gaza - jeshi la Israeli

Msemaji wa jeshi la Israel amesema kuwa mafuta hayataruhusiwa katika Ukanda wa Gaza kama sehemu ya maagizo kutoka kwa uongozi wa kisiasa wa Israel.

Katika taarifa yake, msemaji wa jeshi la Israel Avichay Adraee alidai: "Hali ya kibinadamu katika Ukanda wa Gaza imedhibitiwa."

"Tunawaomba wakaazi wa Ukanda wa kaskazini wa Gaza kwenda kusini," msemaji huyo alisema, akiongeza kwamba "msaada wa kibinadamu utaingia huko na tutaendelea kuzidisha mashambulio kaskazini mwa Ukanda wa Gaza."

"Chini ya maagizo kutoka ngazi ya kisiasa, chakula, dawa na maji vilisafirishwa kupitia kivuko cha Rafah," alisema.

11:00 GMT - Idadi ya vifo katika Ukanda wa Gaza kutokana na mashambulizi ya Israel yafikia zaidi ya 4,300

Wizara ya afya ilisema Jumamosi kuwa watoto 1,756 ni miongoni mwa watu waliouawa katika mashambulizi ya Israel.

10:00 GMT - Viongozi wa Kiarabu wanashutumu mashambulizi ya Israeli dhidi ya Gaza

Viongozi wa nchi za Kiarabu wamelaani mashambulizi ya wiki mbili ya Israel dhidi ya Gaza na kutaka juhudi ziongezwe upya ili kufikia suluhu ya amani ya Mashariki ya Kati ili kukomesha mzunguko wa miongo kadhaa wa ghasia kati ya Waisraeli na Wapalestina.

Akiongea Jumamosi kwenye Mkutano wa Amani wa Cairo, Mfalme Abdullah wa Jordan alikashifu kile alichokiita ukimya wa kimataifa kuhusu mashambulio ya Israel kwenye eneo hilo na kuhimiza kuwepo kwa usawa katika mzozo wa Israel na Palestina.

"Ujumbe ambao ulimwengu wa Kiarabu unasikia ni kwamba maisha ya Wapalestina hayana umuhimu kuliko yale ya Israeli," alisema, akiongeza kuwa alikasirishwa na kuhuzunishwa na vitendo vya unyanyasaji vinavyofanywa dhidi ya raia wasio na hatia huko Gaza, Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan na Israel.

"Uongozi wa Israel lazima utambue mara moja kwamba taifa haliwezi kamwe kustawi ikiwa limejengwa juu ya msingi wa dhuluma. Ujumbe wetu kwa Waisraeli unapaswa kuwa tunataka mustakabali wa amani na usalama kwa ajili yenu na Wapalestina. "

Mkutano wa Cairo unajaribu kutafuta njia za kumaliza vita vya kikanda.

Rais wa Palestina Mahmoud Abbas alisema Wapalestina hawatatawanywa au kufukuzwa katika ardhi yao.

"Hatutaondoka, hatutaondoka," aliambia mkutano huo.

0724 GMT - Malori yaliyokuwa yamebeba misaada ya kibinadamu kutoka Misri kuelekea Gaza iliyozingirwa yalianza kupita kwenye kivuko cha mpaka cha Rafah, chanzo cha usalama na afisa wa Red Crescent ya Misri aliiambia AFP.

Zaidi ya malori 200 yaliyokuwa yamebeba takriban tani 3,000 za msaada yalikuwa yamewekwa karibu na kivuko hicho kwa siku kadhaa kabla ya kuelekea Gaza. Mwanahabari wa Associated Press aliona lori hizo zikiingia.

Wengi huko Gaza, wameishia kula mlo mmoja kwa siku na bila maji ya kutosha ya kunywa, wanasubiri kwa hamu msaada huo.

Wafanyikazi wa hospitali pia walikuwa wakihitaji msaada wa haraka wa vifaa vya matibabu na mafuta kwa jenereta zao kwani wanatibu idadi kubwa ya watu waliojeruhiwa katika milipuko ya mabomu.

Mamia ya watu wanaomiliki hati za kusafiria za kigeni pia walisubiri kuvuka kutoka Gaza hadi Misri ili kuepuka mzozo huo.

Televisheni ya taifa ya Misri ilionyesha malori kadhaa yakiingia langoni katika siku ya 15 ya vita vya Israel dhidi ya Gaza.

0310 GMT - Israeli inaashiria kutositishwa kwa mashambulizi huko Gaza baada ya Hamas kuwaachiulia baadhi ya mateka

Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu aliapa "kupigana hadi ushindi" akiashiria kutosimama katika mashambulizi ya kijeshi ya jeshi lake na uvamizi unaotarajiwa wa Gaza.

Hamas ambayo inatawala Gaza mnamo Ijumaa iliwaachilia Wamarekani Judith Tai Raanan, 59, na bintiye Natalie, 17, ambao walitekwa nyara katika shambulio lake kusini mwa Israeli mnamo Oktoba 7.

Picha iliyopatikana na shirika la habari la Reuters baada ya kuachiliwa kwao ilionyesha wanawake hao wawili wakiwa wamezingirwa na wanajeshi watatu wa Israel na wakishikana mikono na Gal Hirsch, mratibu wa Israel wa mateka na na waliokutoweka.

Malori ya kubeba misaada ambayo Umoja wa Mataifa unaita "mstari wa maisha" bado yamekwama kwenye upande wa Misri wa mpaka wa Rafah kuingia Gaza, ingawa Biden alisema harakati zinaweza kuanza "saa 24 hadi 48 zijazo".

0652 GMT - Shirika la Umoja wa Mataifa linasema wafanyakazi 17 waliuawa tangu kuanza kwa vita 'vibaya' vya Gaza

"Hadi sasa, wenzetu 17 wamethibitishwa kuuawa katika vita hivi vikali. Cha kusikitisha sana, huenda idadi halisi ikaongezeka," UNRWA ilisema katika taarifa yake.

0647 GMT - Israeli inawahimiza raia wake kuondoka mara moja Misri, Jordan

Israel inatoa wito kwa raia wake kuondoka mara moja Misri na Jordan, baraza la usalama la taifa lilisema huku mvutano wa kikanda ukipamba moto kuhusu vita huko Gaza.

"Baraza la Usalama la Kitaifa la Israeli limetoa onyo ya kusafiri Misri (pamoja na Sinai) na Jordan hadi kiwango cha 4 (tishio kubwa): pendekezo la kutosafiri kwenda nchi hizi na kwa wale wanaokaa huko kuondoka haraka iwezekanavyo," baraza hilo lilisema katika taarifa.

0500 GMT - Misri inaandaa mkutano maalum na viongozi wa kanda, maafisa wa Magharibi

Misri inawakaribisha makumi ya viongozi wa kanda na maafisa wakuu wa nchi za Magharibi kwa ajili ya mkutano kuhusu vita kati ya Israel na makundi ya Wapalestina huko Gaza.

Mkutano huo katika mji mkuu mpya wa utawala wa Misri, Mashariki mwa Cairo, utajadili njia za kukomesha mapigano na kutafuta kusitishwa kwa mapigano huku kukiwa na wasiwasi unaoongezeka kuhusu mzozo wa kikanda, vyombo vya habari vya serikali ya Misri viliripoti.

Miongoni mwa waliohudhuria mkutano huo ni viongozi wa Qatar, Umoja wa Falme za Kiarabu na Mamlaka ya Palestina.

0454 GMT - Mwanajeshi wa Israeli waliuawa, 3 kujeruhiwa na kombora dhidi ya kifaru kwenye mpaka wa Lebanon.

Askari wa akiba wa Israel aliuawa na wengine watatu kujeruhiwa na kombora la kifaru karibu na mpaka na Lebanon, jeshi la Israel lilisema.

TRT World