| Swahili
AFRIKA
2 dk kusoma
DRC yapanga kupeleka walinzi maalum kulinda maeneo ya uchimbaji madini
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), ikiwa katika juhudi za kupunguza wizi na uporaji wa madini yake, Jumatatu ilitangaza mpango wa kuanzisha kikosi maalum kitakachohusika na kulinda sekta ya madini nchini humo.
DRC yapanga kupeleka walinzi maalum kulinda maeneo ya uchimbaji madini
DRC inalenga kuwa na zaidi ya walinzi 20,000 wa migodi katika majimbo yote yenye shughuli za uchimbaji ifikapo mwaka 2028./ / AA

Kulingana na taarifa ya Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Migodi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, kikosi hicho kitakachojulikana kama “walinzi wa migodi” kitakuwa na jukumu la kuhakikisha usalama katika mnyororo mzima wa uchimbaji madini.

Hii inajumuisha kulinda maeneo ya migodi na kuhakikisha usafirishaji salama wa madini kutoka maeneo ya uchimbaji hadi vituo vya uchakataji na mipaka ya nchi.

Serikali imetenga uwekezaji wa takribani dola milioni 100 za Marekani kwa ajili ya mafunzo ya miezi sita kwa waajiriwa wapya pamoja na kuwapatia vifaa maalum vinavyohitajika.

Kundi la kwanza la maafisa kati ya 2,500 hadi 3,000 linatarajiwa kupelekwa katika majimbo 22 ya nchi, huku mafunzo yao yakipangwa kufanyika kuanzia Juni hadi Disemba mwaka huu.

Ulinzi wa maeneo makuu ya uchimbaji, hususan katika maeneo ya Greater Katanga na Grande Orientale, unatarajiwa kufikiwa kikamilifu ifikapo mwisho wa mwaka 2027.

Serikali pia inalenga kuwa na zaidi ya walinzi 20,000 wa migodi katika majimbo yote yenye shughuli za uchimbaji ifikapo mwaka 2028.

Sehemu kubwa ya rasilimali za madini za Congo ziko mashariki mwa nchi, eneo ambalo limekumbwa na ukosefu wa usalama kwa muda mrefu. Kwa miaka mingi, utajiri wa madini nchini humo umekuwa chanzo cha migogoro kati ya makundi yenye silaha.

DRC ndiyo mzalishaji mkubwa zaidi wa coltan duniani, na sehemu kubwa ya madini hayo hutoka migodini karibu na Rubaya, mashariki mwa nchi—eneo ambalo lilitekwa na waasi wa M23 mapema mwaka 2024.

Serikali inatarajia mpango huu utaimarisha udhibiti wa mnyororo wa madini, kupambana na biashara haramu ya madini na kuboresha usimamizi wa sekta hii muhimu kwa uchumi wa taifa.

Mkuu wa Ukaguzi wa Migodi, Rafael Kabengele, alisema kuwa lengo ni “kusafisha sekta nzima ya madini kwa kuondoa vitendo vinavyokwenda kinyume na utawala bora, uwazi na ufuatiliaji wa asili ya madini.”

CHANZO:AA