| Swahili
AFRIKA
2 dk kusoma
Benki Kuu Uganda yaonya kuhusu mswada mpya unavyoweza kuhatarisha akiba ya fedha za kigeni
Kwa kiasi fulani mswada unapendekeza kwamba yeyote anayetaka kupokea ufadhili wa kigeni unaozidi Dola za Marekani 106,300 ndani ya miezi 12 anahitaji idhini ya maandishi ya awali kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Ndani.
Benki Kuu Uganda yaonya kuhusu mswada mpya unavyoweza kuhatarisha akiba ya fedha za kigeni
Gavana wa Benki Kuu ya Uganda Michael Atingi-Ego Picha: @BOU_Official / Public domain

Benki Kuu ya Uganda ina wasiwasi kuwa sheria inayopendekezwa yenye lengo la kuzuia ushawishi wa nje katika siasa inaweza kupunguza akiba yake ya fedha za kigeni na kusababisha shinikizo la mfumko wa bei.

Mswada huo unaoitwa "The Protection of Sovereignty Bill, 2026" uliwasilishwa bungeni 15 Aprili 2026.

Kwa kiasi fulani unapendekeza kwamba yeyote anayetaka kupokea ufadhili wa kigeni unaozidi Dola za Marekani 106,300 (takriban UGX 400 milioni) ndani ya miezi 12 anahitaji idhini ya maandishi ya awali kutoka kwa Waziri wa Mambo ya Ndani.

Ikipitishwa sheria itahitaji raia yeyote anayepokea pesa kutoka nje ya nchi kujiandikisha kama wakala wa kigeni, na kupewa cheti kutoka serikali na kufichua fedha zote zinazoingia miongoni mwa masharti mengine.

"Uwezo wa Mswada huu kuyumbisha usawa wa fedha za kigeni katika akiba ya serikali ndio jambo tunalohofia kama Benki Kuu," Gavana wa Benki Kuu Michael Atingi-Ego aliiambia kamati ya bunge ambayo kwa sasa inafanya mikutano ya hadhara kuhusu sheria iliyopangwa.

Benki pia ilichapisha taarifa za Gavana kwenye akaunti yake ya X.

Gavana alionya kuwa utekelezaji wa sheria hiyo utapunguza mtiririko wa kifedha nchini.

"Kwa mfano, mwaka wa fedha uliopita salio la jumla la ziada ya malipo lilikuwa Dola bilioni 1.5. Hivyo ndivyo tulivyoweza kuongeza hifadhi yetu kwa Dola bilioni 1.5. Leo hii tunapozungumza hifadhi zetu zinakaribia Dola bilioni 6. Kwa nini? Kwa sababu mapato haya yamekuwa yakiingia. Unapovuruga mapato haya hapa, tuna hatari ya kupungua kwa akiba yetu na hilo ni janga la kiuchumi kwa nchi," aliongeza.

"Kwa sababu ya kushuka kwa thamani ya sarafu ambayo inaweza kutokea kama matokeo yasiyotarajiwa ya mswada huu...mfumko wa bei utaongezeka kushuka kwa kiwango cha ubadilishaji wa fedha,"Gavana aliongezea.

Benki ya Dunia pia imepinga sheria inayopendekezwa ikisema sheria hiyo inaweza kuleta hatari ya uhalifu katika shughuli zake za maendeleo nchini.

Pendekezo la kuundwa kwa sheria hiyo pia limepokea ukosoaji mkubwa kutoka kwa mashirika ya misaada, benki za biashara, wanaharakati wa haki na upinzani wa kisiasa lakini serikali imepuuza hofu yao ikidai sheria hiyo haina madhara.

CHANZO:TRT Swahili