Rais wa Cameroon Paul Biya amesema Jumatano katika hotuba yake mbele ya Papa kwamba "ulimwengu unahitaji ujumbe wa amani" ambao umeletwa na Papa Leo XIV.
Ziara ya Papa ya nchi nne za Afrika, imeanza huku kukiwa na kauli kutoka kwa Rais wa Marekani Donald Trump kwamba yeye "sio mfuasi mkubwa" wa Papa Leo.
Kauli hii imekuja baada ya Papa Leo ambae ni mzawa wa nchini Marekani kutaka amani Mashariki ya Kati.
"Ulimwengu unahitaji ujumbe wa amani, haki, uvumilivu, kusameheana, na upendo," amesema Rais wa Cameroon.
Bila kumtaja Trump au mapigano ya Iran, Biya amesema "safari ya kitume ya Papa nchini Cameroon inafanyika katika kipindi kigumu kimataifa."
Mkwaruzano wa Papa na Trump
Mgogoro kati ya Marekani na Iran unapoendelea, Papa Leo amekuwa akipaza sauti ya amani, na kuviita vitisho vya Trump alivyovitoa mapema mwezi Aprili dhidi ya Iran kama "visivyokubalika."
Kwa upande wake, Rais Trump kupitia mitandao ya kijamii amemshambulia Papa, ambae awali pia aliukosoa utawala wa Trump dhidi ya sera zake ya uhamiaji.
Mbali na Trump, Makamu wa Rais wa Marekani JD Vance – ambae ni Mkatoliki, ameingilia kati, na kuitaka Vatican "kujihusisha na mambo ya kiroho...na imuache Rais wa
Marekani kuamua kuhusu sera ya umma ya Marekani.














