| Swahili
UTURUKI
3 dk kusoma
Waziri wa Sheria wa Uturuki na Saudi Arabia wakutana kuimarisha ushirikiano katika masuala ya sheria
Mawaziri hao wamejadili kuimarisha ushirikiano katika masuala ya sheria, usalama wa mtandao, akili mnemba na mapambano dhidi ya uhalifu na ugaidi.
Waziri wa Sheria wa Uturuki na Saudi Arabia wakutana kuimarisha ushirikiano katika masuala ya sheria
Waziri wa Sheria wa Uturuki, Akin Gurlek, amekutana na Waziri wa Sheria wa Saudi Arabia, Waleed M. Al-Samaani, jijini Ankara. / / AA

Uturuki na Saudi Arabia zimeahidi kuimarisha ushirikiano katika masuala ya sheria na haki, huku mawaziri wao wa sheria wakijadili ushirikiano wa kisheria na kubadilishana uzoefu katika nyanja mpya zinazoibuka.

Waziri wa Sheria wa Uturuki, Akin Gurlek, amekutana na mwenzake wa Saudi Arabia, Walid Al-Samaani, pamoja na wajumbe wake mjini Ankara, kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Jumatano na Wizara ya Sheria ya Uturuki.

Mawaziri hao wamejadili njia za kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi zao za sheria na haki wakati ambapo uhusiano mpana wa pande mbili unaendelea kukua.

Waziri Gurlek alisema kuwa Uturuki na Saudi Arabia ni nchi ndugu zenye uhusiano wa kina wa kihistoria na kitamaduni, pamoja na wajibu wa pamoja wa kudumisha utulivu wa kikanda.

Amesisitiza kuwa dhamira ya kisiasa ya Rais Recep Tayyip Erdogan na Mwanamfalme Mohammed bin Salman imechangia kugeuza uhusiano wa karibu kati ya nchi hizo kuwa ushirikiano wa vitendo, kufuatia mkutano wao uliofanyika mjini Riyadh mwezi Februari.

"Tunafurahia kuona dhamira hii thabiti ya kisiasa ikizaa matokeo halisi katika sekta mbalimbali, zikiwemo uchumi, biashara, uwekezaji, nishati, ulinzi, utamaduni, utalii, teknolojia, pamoja na sheria na haki. Tunathamini pia kwamba taarifa ya pamoja iliyotolewa baada ya ziara ya Riyadh imesisitiza ushirikiano katika masuala ya sheria na haki. Aidha, kutiwa saini kwa makubaliano ya ushirikiano katika masuala ya sheria na haki wakati wa ziara hiyo ni hatua muhimu kuelekea kuimarisha zaidi uhusiano kati ya wizara zetu," alisema Gurlek.

Katika mkutano huo, Gurlek amesisitiza kuwa Uturuki na Saudi Arabia zinashiriki historia iliyojengwa juu ya kanuni kwamba "dini ya taifa ni haki."

Amesema mataifa yote mawili yanalenga kugeuza maono madhubuti yaliyowekwa na viongozi wao kuwa ushirikiano wa kivitendo katika masuala ya sheria na haki, kwa manufaa ya wananchi wa nchi zote mbili.

"Tuko tayari kushiriki uzoefu wetu"

Waziri Gurlek alisema kuwa maono ya "Karne ya Uturuki" na "Dira ya Saudi 2030" yanasisitiza umuhimu wa kuwa na mifumo ya haki iliyo imara, ya haraka na inayofikika kwa wananchi.

Aliongeza kuwa kuongeza ziara za wajumbe wa pande zote mbili na kuimarisha mawasiliano ya moja kwa moja kati ya wataalamu wa sheria kutachangia kwa kiasi kikubwa kuimarisha uhusiano wa nchi hizo.

Pia ameangazia mfumo wa kidijitali wa mahakama wa Uturuki unaojulikana kama UYAP, unaowezesha taratibu za mahakama kufanyika kwa njia ya kidijitali.

"Tuko tayari kushiriki uzoefu wetu katika uwekaji wa mifumo ya mahakama kidijitali, matumizi ya akili mnemba, usalama wa mtandao, msaada wa kisheria na mbinu mbadala za utatuzi wa migogoro na Wizara ya Sheria ya Saudi Arabia," alisema Waziri huyo.

Waziri huyo pia alitoa wito wa kuongezwa kwa ziara za wajumbe wa pande zote mbili na mawasiliano ya moja kwa moja kati ya wataalamu wa sheria ili kuimarisha ushirikiano.

Gurlek amesisitiza pia umuhimu wa ushirikiano katika kupambana na ufadhili wa ugaidi, uhalifu, uhalifu wa mtandaoni na utakatishaji wa fedha.

Amesema kuwa Uturuki na Saudi Arabia zitaendelea kutetea sheria za kimataifa, haki na utu wa binadamu katika majukwaa ya kikanda na kimataifa.

CHANZO:TRT World and Agencies