Gazeti la Uingereza la The Daily Telegraph limefuta makala inayohusisha kauli za uchochezi kawa Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan baada ya mhariri wake mkuu kukiri kuwa nukuu hizo zilikuwa “za zamani au za kubuniwa.”
Makala hiyo, iliyochapishwa siku ya Jumamosi, Aprili 12, ilidai kuwa Erdogan alikuwa ametishia kuivamia Israel, ikinukuu kauli zilizobuniwa ambazo zilidaiwa kutolewa katika mkutano wa kisiasa.
Ripoti hiyo ilinukuu rais huyo akisema, “Kama tulivyoingia Libya na Karabakh, tunaweza kuingia Israel,” kauli ambazo hazikuwahi kutolewa.
Mhariri mkuu wa Telegraph, Paul Nuki, alitoa taarifa fupi akitambua kosa hilo. “Habari, tumeiondoa habari hiyo. Nukuu hizo zinaonekana kuwa za zamani au zimetungwa. Tunaomba radhi,” aliandika kwenye mitandao ya kijamii.
Tukio hili limeibua upya maswali kuhusu viwango vya uhariri katika mojawapo ya magazeti kongwe ya Uingereza. Ripoti hiyo ilichapishwa wakati wa mvutano mpya Mashariki ya Kati kufuatia makubaliano dhaifu ya kusitisha mapigano—kipindi ambacho upotoshaji wa taarifa unaweza kuwa na madhara makubwa.
Kwa muda, kumekuwepo madai ya baadhi ya vyombo vya habari vya Magharibi kupotosha misimamo ya sera ya nje ya Uturuki na kupotosha kauli za maafisa wake.
Uturuki imekuwa ikitoa wito mara kwa mara kwa vyombo vya habari vya kimataifa kuzingatia viwango vya msingi vya uandishi wa habari vinaporipoti kuhusu Uturuki, ikionya kuwa taarifa za kuzushwa au zilizotolewa nje ya muktadha huchochea hisia hasi dhidi ya nchi hiyo na kudhoofisha juhudi za kidiplomasia katika maeneo yenye hali tete.
Hadi sasa, Telegraph haijatoa marekebisho rasmi zaidi ya ujumbe mfupi wa Nuki kwenye mitandao ya kijamii.














