Makumi ya wataalam wa sheria za kimataifa nchini Marekani wametia saini barua ya wazi wakisema kwamba mashambulizi ya Marekani dhidi ya Iran yanaweza kuwa uhalifu wa kivita, baada ya Rais Donald Trump kusisitiza vitisho vyake wiki hii vya kushambulia mitambo ya Iran ya kuzalisha nishati na kuchuja chumvi.
Zaidi ya wataalam 100 wa sheria za kimataifa nchini Marekani, wakiwemo kutoka vyuo kama vile Harvard, Yale, Stanford na Chuo Kikuu cha California, walisema katika barua hiyo iliyotolewa Alhamisi kwamba mwenendo wa vikosi vya Marekani na matamshi ya maafisa wakuu wa Marekani "unaleta wasiwasi mkubwa kuhusu ukiukaji wa sheria za kimataifa za haki za binadamu na sheria za kimataifa za kibinadamu, ikiwa ni pamoja na uhalifu wa kivita unaoweza kutokea."
Barua hiyo ilibainisha maoni ya Trump katikati ya Machi ambapo alisema Marekani inaweza kufanya mashambulizi dhidi ya Iran "kwa ajili ya kujifurahisha tu." Pia ilitaja maoni kutoka kwa mkuu wa Pentagon Pete Hegseth kutoka mapema Machi ambapo alisema Marekani haipigani kwa kuzingatia "sheria za kijinga za vita."
"Tunawahimiza maafisa wa serikali ya Marekani kuzingatia Mkataba wa Umoja wa Mataifa, sheria za kimataifa za kibinadamu, na sheria za haki za binadamu wakati wote, na kuweka wazi ahadi ya Marekani kwa kuheshimu kanuni za sheria za kimataifa."
Barua hiyo ilichapishwa kwenye tovuti ya jarida la sera ya Just Security.
Wataalam hao walisema 'wana wasiwasi sana kuhusu mashambulio yaliyoangukia shule, vituo vya afya, na nyumba,' wakibainisha shambulio dhidi ya shule moja Iran siku ya kwanza ya vita.
'Matamshi yasio na utu'
Trump siku ya Jumatano alitishia kuipiga Iran "vikali sana."
"Tutawakabili sana katika kipindi cha wiki mbili hadi tatu zijazo. Tutawarudisha kwenye Enzi za Mawe, " Trump alisema.
Kundi kuu la utetezi wa Waislamu nchini Marekani lilionya kwamba matamshi ya Trump wakati wa vita, ikiwa ni pamoja na tishio lake la kuishambulia Iran "kurejea Enzi za Mawe," yamekuwa "ya kudhalilisha."
Vita hivyo vilianza wakati Marekani na Israel zilipoanzisha mashambulizi ya pamoja dhidi ya Iran mnamo Februari 28, na kuua zaidi ya watu 1,340.
Iran ilijibu kwa mashambulizi ya ndege zisizo na rubani na makombora kulenga kambi za Israel na Marekani katika nchi za Ghuba.













