Burundi inatarajiwa kujiunga na mfumo wa malipo wa Afrika Mashariki (EAPS) ifikapo Disemba 2026, hatua itakayorahisisha malipo na biashara kati ya nchi za ukanda huo.
Kati ya mambo mengine, mfumo huo unaowezesha nchi wanachama kufanya miamala ya mipakani kwa sarafu za ndani.
Hadi kufikia sasa, ni mataifa ya Tanzania, Kenya, Uganda na Rwanda ambayo tayari yameunganishwa kwenye mfumo huo.
Burundi, ambayo ilijiunga na Jumuiya ya Afrika Mashariki, Julai 1, 2007, inalenga kujiunga na mfumo wa EAPS, ambao pia huunganisha benki kuu na za kibiashara za nchi wanachama kwa ajili ya miamala mikubwa ya mipakani bila kulazimika kutumia fedha za kigeni, ikiwemo dola ya Marekani.
Hatua hiyo inakuja wakati Jumuiya ya Afrika Mashariki inaendelea kuboresha miundombinu ya kifedha ili kupunguza gharama kubwa za miamala na kurahisisha biashara kwa wajasiriamali wadogo na wa kati.

















