| Swahili
ULIMWENGU
3 dk kusoma
Nchi 20 za Kiislamu zajadili hatua za pamoja dhidi ya ukiukaji wa Israel katika Msikiti wa Al-Aqsa
Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki, Hakan Fidan, amesisitiza nafasi ya kihistoria na kisheria ya Jordan kama mlinzi na msimamizi wa maeneo matakatifu yaliyoko katika Jerusalem Mashariki inayokaliwa.
Nchi 20 za Kiislamu zajadili hatua za pamoja dhidi ya ukiukaji wa Israel katika Msikiti wa Al-Aqsa
Fidan alisema walioshiriki mkutano huo walijikita kikamilifu katika hatua za hivi karibuni za Israel zinazolenga Msikiti wa Al-Aqsa./ / AA

Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki, Hakan Fidan, amesema kuwa karibu nchi 20 za Kiislamu zimejadili “hatua za pamoja” dhidi ya ukiukaji wa hivi karibuni unaofanywa na Israel katika Msikiti wa Al-Aqsa, wakati wa mkutano wa mawaziri kuhusu Jerusalem uliofanyika jijini Amman, Jordan, Jumatano. Amesisitiza kuwa migogoro ya kikanda haipaswi kuondoa umakini wa dunia kutoka kwenye matukio yanayojiri katika maeneo ya Palestina yanayokaliwa.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya mkutano huo, na kujibu swali la Shirika la Habari la Anadolu, Fidan amesema walioshiriki mkutano huo walijikita hasa katika hatua za hivi karibuni za Israel zinazolenga Msikiti wa Al-Aqsa.

“Leo tumeshiriki katika mkutano wa kihistoria kabisa jijini Amman,” alisema Fidan. Aliongeza: “Kulikuwa na majadiliano makubwa ya maoni. Nchi mashuhuri za ulimwengu wa Kiislamu zilieleza wasiwasi wao pamoja na hasira zao, huku pia zikijadili hatua za vitendo, za kidiplomasia na nyinginezo zinazopaswa kuchukuliwa.”

Amesema kuwa vita vinavyoendelea katika Ghuba, athari za kikanda na kimataifa zinazotokana na kufungwa kwa Mlango-Bahari wa Hormuz, pamoja na mabadiliko ya mwelekeo wa umakini wa kimataifa, havikuondoa umakini wa washiriki kuhusu “suala la Palestina, Msikiti wa Al-Aqsa, Gaza na Ukingo wa Magharibi.”

“Kwa sababu tunafahamu kwamba ikiwa umakini wetu utaelekezwa kwenye suala moja pekee, Israel itapata urahisi zaidi wa kuendeleza kile inachofanya huko Gaza, katika Msikiti wa Al-Aqsa, kuhusu suala la Jerusalem na katika Ukingo wa Magharibi,” alisema.

Fidan alirudia kusisitiza nafasi ya kihistoria na kisheria ya Jordan kama mlinzi na msimamizi wa maeneo matakatifu katika Jerusalem Mashariki inayokaliwa, na kusema kuwa Uturuki inaichukulia Al-Aqsa kama sehemu mojawapo ya maeneo yake matakatifu.

“Rais wetu (Erdogan), serikali yetu, taifa letu na jamii yetu wanautazama Msikiti wa Al-Aqsa kama mojawapo ya maeneo yetu matakatifu. Ukiukaji wowote unaolenga eneo hilo unachukuliwa kuwa ni ukiukaji dhidi ya maadili ya taifa letu,” alisema Fidan.

Aliongeza kuwa Uturuki na Jordan zilitoa ujumbe wa mshikamano kuhusu Jerusalem na Al-Aqsa wakati wa mkutano huo.

Muungano wa nchi nne wajadii mpango wa amani wa Gaza na dira ya kikanda

Fidan pia alisema alihudhuria mkutano wa tano wa mawaziri wa “Muungano wa Nne”, unajumuisha Saudi Arabia, Uturuki, Misri na Pakistan, ambapo mawaziri walijadili maendeleo kuhusu Gaza na juhudi za kutekeleza mpango wa amani.

Alisema nchi hizo nne zimekuwa zikifanya kazi kwa bidii kuendeleza mpango huo, huku akibainisha kuwa Misri na Uturuki zinaendelea kutekeleza nafasi za upatanishi.

Mawaziri hao pia walijadili kile Fidan alichokiita mtazamo wa Israel kuhusu mchakato wa amani.

“Tulijadili kwa kina jinsi ya kukabiliana na mienendo ya Israel, kupuuza kwake sheria za kimataifa, na kutofuata kwake kanuni wakati wa utekelezaji wa mpango wa amani,” alisema.

Fidan alisema mawaziri hao walifikia maamuzi kadhaa ambayo yatawasilishwa kwa viongozi wa nchi zao, akiongeza: “Katika siku zijazo mtaona hatua zinazohusiana na maamuzi hayo.”

Alisema mkutano huo pia ulijadili mvutano mpana wa kikanda, ikiwemo hatari zinazohusishwa na migogoro hiyo, hali ya kutokuwa na utulivu inayohusishwa na Bahari Nyekundu, na uwezekano wa kuongezeka zaidi kwa mzozo.

Fidan alisema nchi hizo nne pia zilitathmini waraka wa dira ya kikanda ambao zimekuwa zikiuandaa kwa pamoja, akieleza kuwa ni mfumo wa awali unaolenga kutoa suluhisho la kudumu kwa changamoto za muda mrefu katika eneo hilo.

“Hii itakuwa hatua ya kwanza kuelekea kuweka mfumo wa kutatua kabisa matatizo yanayoikabili kanda hii,” alisema. “Kwa kukamilisha kazi hii kwa utaratibu, tunatarajia kujenga utulivu wa kudumu wa kikanda, usalama na amani hatua kwa hatua.”

CHANZO:AA