Nairobi imewasilisha rasmi ombi lake la kuandaa Mashindano ya Dunia ya Riadha ya mwaka 2029, katika juhudi za kuleta tukio kubwa zaidi la kimataifa la mchezo huo barani Afrika kwa mara ya kwanza.
Mji mkuu wa Kenya unashindania fursa hiyo na London, Roma na Munich kupata haki ya kuandaa mashindano hayo, huku Shirikisho la Riadha Duniani likitarajiwa kutangaza mji utakaoshinda mwezi Septemba.
Serikali ya Kenya imeahidi kuunga mkono kikamilifu ombi hilo, ikiwemo kutoa miundombinu, usalama na usaidizi wa kiutawala unaohitajika ili kuendesha mashindano hayo.
Kenya ina rekodi nzuri ya kuandaa mashindano makubwa ya riadha, baada ya kuandaa Mashindano ya Dunia ya Mbio za Nyika mjini Mombasa mnamo 2007, Mashindano ya Dunia ya wanariadha chini ya miaka 18 jijini Nairobi mnamo 2017 na Mashindano ya Dunia ya wanariadha chini ya miaka 20 katika mji mkuu mnamo 2021.
Nairobi pia iliandaa Mashindano ya Riadha ya Afrika mnamo 2010.
Ombi hili likifanikiwa litakuwa wakati muhimu kwa riadha ya Afrika. Licha ya kutawala kwa bara hilo katika mbio za masafa marefu na historia yake ndefu ya kutoa mabingwa wa dunia na Olimpiki, Afrika haijawahi kuandaa Mashindano ya Riadha ya Dunia ya wataalamu.
Kenya hapo awali imejaribu kupata fursa hiyo ikiwa ni pamoja na ombi la 2025, ambalo hatimaye lilitolewa kwa Tokyo.
Kwa hivyo, shindano la 2029 linawakilisha fursa nyingine kwa Kenya kujiweka sio tu kama nguvu ya vipaji vya riadha, lakini pia kama mwenyeji mkuu wa matukio ya michezo ya kimataifa. Uamuzi huo sasa unatarajiwa mweziSeptemba.


















