| Swahili
ULIMWENGU
3 dk kusoma
Iran yaonya Korea Kusini dhidi ya kutuma vikosi vya kijeshi katika Mlango-Bahari wa Hormuz
Iran imesema ushiriki wowote wa kijeshi wa Korea Kusini katika juhudi za kuhakikisha usalama wa usafiri wa meli kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz utakuwa na madhara makubwa.
Iran yaonya Korea Kusini dhidi ya kutuma vikosi vya kijeshi katika Mlango-Bahari wa Hormuz
Wanajeshi wa Korea Kusini wanashiriki katika mazoezi makubwa ya kijeshi ya pamoja kati ya Korea Kusini na Marekani jijini Seoul, Agosti 19, 2026./ / AFP

Iran imeionya Korea Kusini kwamba kushiriki kwake kijeshi kwa njia yoyote katika eneo la Ghuba na Mlango-Bahari wa Hormuz utakuwa na “madhara makubwa”, huku kukiwa na taarifa kwamba Korea Kusin inazingatia kutuma vikosi katika juhudi za kimataifa za kuhakikisha usalama wa usafiri wa meli kupitia njia hiyo muhimu ya kimkakati.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmaeil Baqaei, amesema Jumatatu kwamba uhusiano kati ya Iran na Korea Kusini umeendelea kwa zaidi ya miaka 64, kwa msingi wa kuheshimiana.

Baqaei amesema Iran inathamini uhusiano wake na Korea Kusini, lakini akaonya kwamba uwepo wowote wa kijeshi wa kigeni katika Ghuba au Mlango wa Hormuz utachukuliwa kama msaada wa moja kwa moja kwa Marekani.

Amesema Iran inajilinda dhidi ya kile alichokiita uchokozi wa Marekani na inajibu kile alichokitaja kuwa “uhalifu wa kivita wa Marekani dhidi ya wanawake na watoto”.

"Hakuna nchi huru na yenye kuwajibika inapaswa kukubali shinikizo na vitisho vya Marekani," Baqaei amesema kwenye mtandao wa X.

Korea Kusini yatathmini uwezekano wa kutuma vikosi

Wizara ya Mambo ya Nje ya Korea Kusini ilisema Jumatatu kwamba nchi hiyo inaendelea kuwasiliana na jamii ya kimataifa, kuhusu kurejesha utulivu Mashariki ya Kati na kuhakikisha meli zinapita kwa uhuru kupitia Mlango wa Hormuz.

Shirika la habari la Yonhap, likinukuu vyanzo vya kidiplomasia, liliripoti kwamba Korea Kusini imeendelea kuwa na mawasiliano ya wazi na Iran wakati majadiliano kuhusu uwezekano wa kutuma vikosi yakiendelea.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Rais wa Marekani Donald Trump ameongeza shinikizo kwa Korea Kusini ili ichangie katika juhudi za kuhakikisha usalama wa usafiri wa meli kupitia mlango huo.

Afisa mmoja katika Ikulu ya Korea Kusini alisema Ijumaa kwamba hakuna uamuzi wa mwisho uliokuwa umefikiwa, na kwamba tathmini bado inaendelea.

Afisa huyo alisema nchi hiyo inaweza kuzingatia kuchangia katika juhudi za kimataifa za kuhakikisha uhuru wa usafiri wa meli, mradi hatua hiyo isiathiri utayari wa Korea Kusini wa kujilinda.

Kituo cha televisheni cha nchini humo, SBS, kiliripoti kwamba maandalizi yalikuwa yakiendelea kwa ajili ya uwezekano wa kutumwa kwa kikosi kitakachohusisha ndege za doria za baharini aina ya P-8, timu ya wataalamu wa kutegua mabomu na mabaki ya vilipuzi, pamoja na meli ya kusaidia usafirishaji wa vifaa.

Uamuzi wowote wa kutuma vikosi utahitaji idhini ya Baraza la Usalama la Taifa la Korea Kusini na Baraza la Mawaziri, pamoja na ridhaa ya Bunge la Taifa.

Korea Kusini ni mshirika wa Marekani chini ya mkataba wa ulinzi, na kwa mujibu wa Trump, takribani wanajeshi 39,000 wa Marekani wamewekwa katika Rasi ya Korea.

CHANZO:Anadolu Agency