Huko nchini Ujerumani, stori kubwa kwa sasa ni Marie-Louise Eta.
Mwanamama huyu ameteuliwa kuifundisha timu ya soka ya wanaume ya Union Berlin inayoshiriki Ligi Kuu ya Ujerumani, maarufu kama Bundesliga.
Kocha huyo mwenye umri wa miaka 34, anaingia kwenye vitabu vya historia, kwa kuwa mwanamke wa kwanza katika ligi kuu tano bora barani Ulaya, kufundisha timu ya soka ya wanaume.
Marie-Louise Eta amepewa jukumu la kuiongoza klabu ya Union Berlin kwa miezi miwili, mpaka Juni mwaka huu.
Uamuzi wa kumpa mikoba mwanamama huyu jukumu hilo kubwa, linafuatia mechi ya hivi karibuni, ambapo Union Berlin ilipoteza kwa mabao 3-1 dhidi ya Heidenheim, na klabu hiyo kulazimika kumtimua aliyekuwa kocha wake, Steffen Baumgart.
Kibarua kinachomsubiri Marie-Louise Eta kwa sasa, ni kuinasua Union Berlin kutoka nafasi yake ya 11 kwenye msimamo wa Bundesliga.
Hata hivyo, hilo si jambo geni kwa bara la Afrika.
Mwaka 2024, Jackline Juma alikuwa mwanamke wa kwanza kufundisha timu ya soka ya wanaume, baada ya kuiongoza klabu ya Talanta, iliyokuwa ikishiriki ligi kuu ya KPL nchini Kenya.
Mwaka huo huo, Oliver Mbekeka alipewa jukumu la kuifundisha klabu ya Lugazi iliyokuwa ikishiriki ligi kuu ya nchini Uganda, na kuwa mwanamke wa kwanza nchini humo kufundisha timu ya wanaume.
Oliver alichukua mikoba hiyo kufuatia kuondoka kwa kocha Sadiq Ssempigi na atakumbukwa kwa kuiongoza Lugazi kuifunga klabu ya Express kwa bao 1-0 kwenye uwanja wa Nakivubo.















