| Swahili
ULIMWENGU
3 dk kusoma
Iran yakataa pendekezo la usitishaji mapigano la Marekani lililowasilishwa na Iraq: ripoti
Iran imekataa pendekezo la Marekani la usitishaji mapigano lililowasilishwa na Waziri Mkuu wa Iraq, Ali al-Zaidi, ambaye hivi karibuni amekutana na Rais wa Marekani Donald Trump katika Ikulu ya White House, kwa mujibu wa gazeti la The New York Times.
Iran yakataa pendekezo la usitishaji mapigano la Marekani lililowasilishwa na Iraq: ripoti
Rais wa Iran Masoud Pezeshkian amekutana na Waziri Mkuu wa Iraq Ali al-Zaidi jijini Tehran, Iran, tarehe 22 Julai 2026. / / AP

Gazeti la The New York Times, likinukuu maafisa wa Iran na Iraq wenye ufahamu wa suala hilo, linasema al-Zaidi aliwasilisha pendekezo hilo wakati wa ziara yake jijini Tehran baada ya kukutana na Trump.

Ingawa maelezo kamili ya pendekezo hilo hayakuwekwa wazi, maafisa wa Iran walisema ndilo pendekezo pekee ambalo Marekani imewasilisha hadi sasa.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Iran imekataa kwa sababu pebdekezo hilo halikutoa suluhisho kuhusu suala la udhibiti wa Mlango-Bahari wa Hormuz.

Ziara ya al-Zaidi ilikuwa ya kwanza rasmi nchini Iran tangu alipoingia madarakani mwezi Mei. Aliambatana na ujumbe wa ngazi ya juu wa mawaziri na kukutana na Rais wa Iran, Masoud Pezeshkian. Pande hizo mbili zimejadili uhusiano wa pande mbili, maendeleo ya kikanda na juhudi za kuimarisha usalama na utulivu.

Maafisa wa Iran wamesema mazungumzo hayo pia yalihusu utekelezaji wa makubaliano yaliyosainiwa awali, huku serikali zote mbili zikisisitiza umuhimu wa kupanua ushirikiano katika biashara, nishati, usafirishaji na masuala ya kikanda.

Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Iran, al-Zaidi pia amekutana na mkuu wa timu ya mazungumzo ya Iran, Spika wa Bunge Mohammad Bagher Ghalibaf, pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje Abbas Araghchi.

Hatari ya vita kupanuka

Ripoti hiyo inaeleza kuwa maafisa wa Iran wanajiandaa kwa uwezekano wa vita kupanuka zaidi ikiwa Trump atatekeleza vitisho vyake vya kushambulia Tehran na miundombinu mingine muhimu.

Kwa mujibu wa The New York Times, maafisa wawili wa Iran wamesema mashambulizi hayo yangeifanya Iran kupanua vita katika eneo zima kwa kulenga Tel Aviv na kuiomba kundi la Wahouthi wa Yemen kufunga Mlango-Bahari wa Bab al-Mandab.

Wakati huo huo, Jeshi la Marekani kupitia Kamandi Kuu ya Marekani (CENTCOM) lilitangaza kuwa limefanya mashambulizi dhidi ya malengo ya Iran kwa usiku wa 13 mfululizo mapema Ijumaa.

Siku ya Jumatano, mamlaka za Iran zilisema mashambulizi yanayoendelea ya Marekani yamesababisha vifo vya watu 53 na kujeruhi wengine 592.

Mvutano katika eneo hilo umeongezeka katika kipindi cha karibu wiki mbili zilizopita baada ya Trump kutangaza Julai 8 kwamba usitishaji mapigano uliokuwa umeainishwa katika hati ya makubaliano ya maelewano kati ya Marekani na Iran ya mwezi uliopita haukuwa tena unatumika.

Tangu wakati huo, Marekani na Iran zimekuwa zikishambuliana, huku Marekani ikilenga maeneo ndani ya Iran na huku Iran ikidai kushambulia vituo vya kijeshi na vifaa vya Marekani katika nchi kadhaa za eneo hilo.

Mapambano hayo yamesababisha usumbufu katika usafirishaji wa meli kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz, kuhatarisha usambazaji wa nishati duniani, kusababisha kufungwa kwa muda kwa baadhi ya anga za nchi mbalimbali, na kuongeza tahadhari kuhusu uwezekano wa mashambulizi dhidi ya vituo na maslahi ya Marekani nje ya Mashariki ya Kati.

CHANZO:TRT World and Agencies