| Swahili
ULIMWENGU
3 dk kusoma
UAE yasitisha shughuli zote za biashara na Iran
Tangazo hilo limetolewa baada ya Wizara ya Ulinzi ya UAE kusema kuwa imegundua makombora mawili ya balistiki ya Iran yaliyolenga usafiri wa baharini.
UAE yasitisha shughuli zote za biashara na Iran
Mvutano kati ya UAE na Iran umeongezeka sana kufuatia mashambulizi ya makombora mawili ya balistiki ya Iran. / / Reuters

Umoja wa Falme za Kiarabu UAE imesitisha shughuli zote za biashara na miamala ya kifedha na Iran “hadi pale itakapotangazwa vinginevyo,” shirika la habari la serikali la UAE, WAM, limeripoti likimnukuu Mkurugenzi wa Mawasiliano ya kimkakati wa Wizara ya Mambo ya Nje.

Kwa sasa, hakuna maelezo zaidi yaliyotolewa kuhusu hatua hiyo. Hata hivyo, tangazo hilo limetolewa muda mfupi baada ya Wizara ya Ulinzi ya UAE kusema kuwa imegundua makombora mawili ya balestiki kutoka Iran yaliyolenga eneo la usafiri wa majini.

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Esmaeil Baghaei, amekanusha taarifa ya UAE kwamba makombora hayo yalirushwa kutoka Iran kuelekea nchi hiyo ya Ghuba, akionya dhidi ya kile alichokiita madai “yasiyo na msingi.”

Katika taarifa iliyochapishwa kwenye chaneli rasmi ya Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran kwenye Telegram, wizara hiyo ilisema: “Kuishutumu Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kunapingana na kanuni ya ujirani mwema na kunazuia juhudi za kujenga uaminifu miongoni mwa nchi za eneo.”

Baghaei pia amezitaka “nchi zote za eneo” kujiepusha na tuhuma zisizo na ushahidi dhidi ya Iran.

Mvutano katika Mashariki ya Kati umeongezeka baada ya Marekani na Israel kufanya mashambulizi ya pamoja dhidi ya Iran.

Iran ilijibu kwa kufanya mashambulizi katika nchi kadhaa za eneo hilo, ikiwemo UAE, ambayo inaandaa vituo na rasilimali za kijeshi za Marekani.

Katikati ya Juni, Iran na Marekani zilitia saini hati ya makubaliano iliyosimamiwa na Pakistan, kwa lengo la kumaliza vita kati yao na kufikia makubaliano ya kudumu ya amani.

Hata hivyo, mazungumzo hayo yamekwama kutokana na mizozo inayoendelea kuhusu masharti ya hati hiyo ya makubaliano pamoja na suala la usafiri kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz, njia muhimu kwa usafirishaji wa nishati duniani.

“Tishio la mashambulizi ya makombora”

Mapema siku hiyo, UAE iliishutumu Iran kwa kurusha makombora mawili ya balestiki kuelekea eneo lake. Hii ilikuwa mara ya kwanza baada ya miezi kadhaa kwa Wizara ya Ulinzi ya UAE kusema kuwa imegundua mfululizo wa makombora yaliyolenga nchi hiyo.

Katika taarifa iliyochapishwa na Wizara ya Ulinzi kwenye mtandao wa X siku ya Jumanne, ilisema: “Mifumo ya ulinzi wa anga ya UAE iligundua makombora mawili ya balestiki yaliyorushwa kutoka Iran kuelekea nchini; kombora la kwanza lilianguka nje ya bahari ya eneo la UAE, huku la pili likianguka ndani ya maji ya eneo la UAE.”

Taarifa hiyo ilitolewa takriban saa mbili baada ya ujumbe mfupi wa tahadhari kutumwa kwenye simu za wakazi wa UAE, ukiwaonya kuhusu “tishio la mashambulizi makombora.”

“Kwa sababu ya hali ya sasa na uwezekano wa tishio la makombora, tafadhali nendeni mara moja mahali salama katika jengo lililo karibu lenye ulinzi,” Wizara ya Mambo ya Ndani ilisema katika ujumbe huo. Tahadhari hiyo iliondolewa muda mfupi baadaye.

Ilikuwa mara ya kwanza kwa tahadhari ya aina hiyo kutolewa tangu tahadhari iliyotolewa mwezi Juni, na tahadhari nyingine iliyotolewa mwezi Julai kuhusu shambulizi ambalo hatimaye halikuingia katika eneo la UAE.

Kabla ya hapo, tahadhari ya mwisho kuhusu makombora ilikuwa imetolewa mwanzoni mwa Mei.

CHANZO:TRT World and Agencies