| Swahili
AFRIKA
2 dk kusoma
Kaka mkubwa wa mfalme mpya wa Tooro, afariki
Inaripotiwa kuwa mwana wa mfalme huyo alikuwa akipambana na saratani kwa zaidi ya mwaka mmoja.
Kaka mkubwa wa mfalme mpya wa Tooro, afariki
David Kijanangoma Araali, kaka wa mfalme mpya wa Tooro aliugua saratani ya koo kwa zaidi ya mwaka mmoja

Mwana wa Mfalme David Kijanangoma Araali, kaka mkubwa wa Mfalme mpya aliyeteuliwa wa Ufalme wa Tooro nchini Uganda, amefariki dunia baada ya kuugua kwa muda mrefu ugonjwa wa saratani ya koo.

Kijanangoma alifariki dunia siku ya Jumanne katika Taasisi ya Saratani ya Uganda iliyoko Mulago, Kampala, ambako alikuwa akipatiwa matibabu.

Kifo chake kilithibitishwa na maafisa wa Ufalme wa Tooro.

Inaripotiwa kuwa mwana wa mfalme huyo alikuwa akipambana na saratani kwa zaidi ya mwaka mmoja. Mwezi Aprili, familia yake na marafiki walitoa wito wa msaada wa kifedha, wakisema alihitaji takriban shilingi za Uganda milioni 700 ili kupata matibabu maalum nchini India baada ya kutumia akiba yake binafsi kwa matibabu nchini Uganda.

Kifo chake kinakuja siku chache tu baada ya mdogo wake, Mwana Mfalme Edward Rukidi Kijanangoma, kutangazwa kuwa Mfalme mpya wa Tooro kufuatia kifo cha Mfalme Oyo Nyimba Kabamba Iguru Rukidi IV mwezi uliopita.

Edward Kijanangoma alichaguliwa na ukoo wa Babiito kuwa mrithi wa Oyo, ambaye alifariki dunia akiwa na umri wa miaka 34 baada ya kupata matibabu ya saratani nchini Marekani.

Hata hivyo, uteuzi wake umepingwa na baadhi ya wanafamilia wa marehemu mfalme, wakidai kuwa Oyo aliacha wosia uliomtaja mwanawe wa kumzaa kuwa mrithi.

Hivyo, kifo cha Mwana wa Mfalme David kinakuja katika wakati nyeti kwa familia ya kifalme ya Tooro, ambayo tayari inakabiliwa na mzozo wa kurithi ufalme kufuatia kifo na mazishi ya Mfalme Oyo.

Kijanangoma alikuwa mwanachama wa familia ya kifalme ya Babiito na kaka mkubwa wa mfalme mpya aliyeteuliwa.

Kifo chake kinaongeza pigo jingine kwa familia hiyo ya kifalme ambayo imekuwa ikiomboleza kifo cha Mfalme Oyo, aliyetawala Tooro kwa zaidi ya miongo mitatu baada ya kupanda kiti cha enzi akiwa na umri wa miaka mitatu mnamo mwaka 1995.

Maafisa wa Ufalme wa Tooro bado hawajatangaza mipango kamili ya mazishi ya Mwana wa Mfalme David.

CHANZO:TRT Afrika and agencies