Na Daniel Morales Ruvalcaba
Kombe la Dunia 2026 linatarajiwa kuwa mashindano makubwa zaidi katika historia ya michuano hiyo. Kwa mara ya kwanza, mashindano hayo yatakuwa na timu 48 na mechi 104 — zaidi kuliko toleo lolote lililopita — zikichezwa katika miji 16 nchini Marekani, Canada, na Mexico.
Upanuzi huu pia unaonekana katika kiwango cha fedha za zawadi. FIFA itagawa zaidi ya Dola milioni 871 kwa timu zitakazoshiriki, huku mabingwa wakipokea Dola milioni 50 — karibu mara mbili ya kiasi kilichotolewa kwa washindi wa Kombe la Dunia 2010 nchini Afrika Kusini.
Ukubwa wa mashindano hayo — pamoja na ushiriki wa mataifa kadhaa yatakayoshiriki kwa mara ya kwanza, ikiwemo Cape Verde, Curaçao, Jordan, na Uzbekistan — umeibua msisimko mkubwa duniani kote, huku zaidi ya maombi milioni 500 ya tiketi tayari yakiwasilishwa.
Mahitaji hayo makubwa yanaonyesha mvuto mkubwa wa kimataifa wa mashindano hayo pamoja na uwezo wake mkubwa wa kuvutia vyombo vya habari duniani.
Wachambuzi wanakadiria kuwa kati ya wageni milioni tano hadi saba kutoka mataifa mbalimbali wanaweza kusafiri kwenda Amerika Kaskazini kwa ajili ya tukio hilo, jambo litakalozalisha athari za kiuchumi zinazozidi Dola bilioni 40.
Kutokana na ukubwa wake, ugumu wa maandalizi, na mfumo mpya, toleo hili la 2026 linatarajiwa kuweka kiwango kipya kwa matukio ya michezo ya kimataifa.
Kwa kuandaliwa kwa ushirikiano wa nchi tatu, mashindano hayo hayatabadilisha tu namna matukio makubwa yanavyoratibiwa na kusimamiwa, bali yanaweza pia kuwa mfano wa mashindano ya kimataifa katika muongo ujao.
Wakati nchi zinaposhirikiana kuandaa mashindano
Wazo la kuandaa kwa pamoja mashindano makubwa ya soka lilianza Julai 1995, wakati UEFA Euro 2000 ilipotolewa kwa Ubelgiji na Uholanzi. Hii ilikuwa mara ya kwanza kwa mashindano makubwa ya bara kuchezwa katika zaidi ya nchi moja.
Mbali na soka, uamuzi huo uliendeshwa pia na sababu za kiutendaji: kugawana majukumu kulisaidia nchi zote mbili kukidhi mahitaji ya miundombinu na usafirishaji huku zikizalisha faida kubwa kwa vyama vyao vya soka.
Chini ya kaulimbiu “Football Without Borders” (Soka Bila Mipaka), mashindano hayo pia yalikuza taswira ya ushirikiano wa nchi mbili na utambulisho wa pamoja wa Ulaya.
Mfumo huo ulirudiwa baadaye katika UEFA Euro 2008, UEFA Euro 2012, na UEFA Euro 2020, ambayo ilichezwa katika miji 12 ya nchi 12 tofauti. Mashindano yajayo pia yatafuata mfumo huo, huku Uingereza na Ireland zikiandaa mwaka 2028, na Italia pamoja na Uturuki kuandaa mwaka 2032.
Kadri muda ulivyopita, kuandaa kwa pamoja kumekuwa zaidi ya mkakati wa kifedha au kiutendaji barani Ulaya, na sasa ni mfano unaotoa faida za kiutawala, kifedha, na pia kuimarisha mshikamano wa kijamii barani humo.
Kwa kiwango cha dunia, kuandaa Kombe la Dunia kwa pamoja kumekuwa jambo nadra. Kombe la Dunia la 2002 lililoandaliwa na Korea Kusini na Japan lilikuwa “uamuzi usio wa kawaida.” Hata hivyo, ushirikiano huo haukutokea kwa hiari bali ulikuwa mkakati wa kupata haki za kuandaa mashindano hayo, kwani nchi zote mbili zilikuwa washindani na ziliweza kuishinda Mexico kwa kuungana.
Hata wakati wa mashindano, mvutano uliendelea kuwepo: mpangilio rasmi wa jina “Korea/Japan” ulizua migogoro ya kidiplomasia, huku ratiba ya mechi na fainali iliyochezwa Yokohama ikionyesha mazungumzo magumu kati ya serikali zote mbili na FIFA.
Kwa hiyo, tofauti na mashindano ya Ulaya, ushirikiano wa Korea-Japan 2002 ulikuwa matokeo ya mazungumzo ya marefu na ulihusisha masuala nyeti ya heshima ya kitaifa.
Kutokana na mifano hiyo, kuna mitazamo miwili tofauti ya kuandaa pamoja tukio kubwa la michezo.
Mfumo wa Ulaya — ulioonekana tangu Euro 2000 — unachanganya maslahi ya kiuchumi na kiutendaji pamoja na simulizi ya mshikamano na ukaribu wa nchi jirani. Kinyume chake, Korea-Japan 2002 iliongozwa zaidi na mantiki ya kivitendo, ambapo ushirikiano ulikuwa njia ya kupata manufaa ya kitaifa na kuongeza hadhi ya kila nchi kimataifa.
Katika muktadha huu, Kombe la Dunia la 2026 linaonekana kuwa katikati ya mifumo hiyo miwili.
Kwa upande mmoja, mashindano haya yana simulizi ya umoja wa kikanda kuliko Korea-Japan 2002, jambo linaloonekana hata katika jina “United” na wazo la zabuni ya pamoja ya nchi tatu za Amerika Kaskazini. Hata hivyo, upande huo wa kiishara unaambatana na maslahi ya kitaifa yaliyo wazi.
Maslahi ya kimkakati
Kwa Marekani, maslahi ya kimkakati katika kuandaa kwa pamoja Kombe la Dunia la 2026 yanachanganya malengo ya michezo na biashara yaliyotokana na Kombe la Dunia la 1994.
Mashindano hayo yaliweka rekodi ya watazamaji wengi zaidi viwanjani — zaidi ya watu milioni 3.5 wakitazama mechi 52 — na yalikuwa kichocheo cha kuanzishwa kwa ligi ya Marekanoi ya Major League Soccer (MLS) mwaka 1996, ambayo sasa ina timu 30 na nyota wa kiwango cha juu kama Lionel Messi.
Msukumo mkubwa wa mkakati huu umetokana na ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi. Hili lilionekana katika ujumbe wa Rais wa Marekani Donald Trump wakati FIFA ilipotangaza rasmi nchi mwenyeji wa Kombe la Dunia la 2026: “Asanteni kwa kuileta Kombe la Dunia Marekani, Mexico, na Canada. Nilifanya kazi kwa bidii katika hili pamoja na timu kubwa ya watu wenye vipaji.
Hatukuwahi kushindwa, na litakuwa Kombe la Dunia kubwa! Shukrani maalum kwa Bob Kraft kwa ushauri wake mzuri.”
Kwa hakika, Bob Kraft, mmiliki wa timu ya New England Patriots, pamoja na wafanyabiashara wengine walishiriki kikamilifu katika zabuni hiyo, wakichangia uzoefu katika masoko ya michezo, matangazo, na usimamizi wa matukio makubwa, kwa lengo la kuiimarisha Marekani kama moja ya masoko yenye faida kubwa katika soka la dunia na kuimarisha MLS kama ligi kubwa.
Nchini Canada, mkazo umewekwa katika kukuza soka kitaifa na kuimarisha taaluma yake. Kwa James Johnson, kamishna wa Premier League ya Canada (CPL), Kombe la Dunia la 2026 ni “fursa ya kuifanya soka kutazama kwa wingi Canada, kuongeza mapato ya kibiashara, na kuiweka CPL katikati ya ajenda ya michezo nchini.”
Hata hivyo, matarajio ya Canada ni zaidi ya michezo. Waziri wa Utalii, Sanaa, Utamaduni na Michezo wa British Columbia, Anne Kang, alisema Machi 2026 kwamba “kutumia mwonekano wa kimataifa wa Kombe la Dunia kutafungua milango ya kuongeza utalii, kuunda ajira, na kuimarisha nafasi yetu kama lango la Canada kuelekea eneo la Asia-Pasifiki.”
Hivyo, kuandaa mashindano hayo kwa pamoja pia kunaonekana kama jukwaa la kuimarisha hadhi ya kiuchumi na utalii wa nchi hiyo duniani.
Kwa upande wa Mexico, Kombe la Dunia la 2026 lina umuhimu wa kipekee wa kihistoria: itakuwa nchi ya kwanza kuandaa Kombe la Dunia la wanaume kwa mara ya tatu, baada ya 1970 na 1986. Hii inaongeza nafasi yake katika historia ya soka duniani.
Mexico 70 inakumbukwa kwa ubingwa wa tatu mfululizo wa Brazil chini ya Pelé, huku Mexico 86 ikikumbukwa kwa chenga za Diego Maradona na ushindi wa Argentina.
Katika matukio yote mawili, nchi hiyo ilishuhudia mafanikio ya wachezaji wawili wanaochukuliwa kuwa miongoni mwa wakali zaidi katika historia ya soka.
Urithi huo wa kihistoria sasa unaunganishwa na mtazamo wa kisasa wa athari za kijamii. Kwa Meya Claudia Sheinbaum, lengo ni “kutumia Kombe la Dunia kuifanya soka kuwa chombo cha amani, michezo, elimu ya mwili, na ujenzi wa jamii.”
Kwa mujibu huo, utawala wake umeanzisha mkakati wa “Social World Cup Mexico 2026,” unaojumuisha zaidi ya shughuli 5,000 za kitamaduni, michezo, na kijamii kote nchini.
Lengo ni kupanua sherehe nje ya viwanja vya michezo, kwa kuhimiza ujumuishaji, mshikamano wa kijamii, na ustawi wa jamii.
Hatua mpya ya Kombe la Dunia 2026
Kwa hiyo, katika mfumo unaochanganya vipengele vya mashindano ya pamoja ya Ulaya na uzoefu wa Korea-Japan 2002, wenyeji hao watatu wameweza kuunganisha maslahi tofauti lakini yanayokamilishana: Marekani inalenga kuimarisha soka kama sekta kubwa ya biashara na kuimarisha MLS; Canada inalenga kupanua nafasi ya soka kiuchumi, kiutalii, na kitamaduni; na Mexico inaongeza uzito wake wa kihistoria na kijamii katika kumbukumbu ya dunia ya mchezo huo.
Kwa pamoja, Kombe la Dunia la United 2026 linaweka Amerika Kaskazini kama moja ya maeneo muhimu zaidi ya soka katika karne ya 21.
Zaidi ya changamoto za kiutawala na maandalizi, mashindano hayo yanaonyesha jinsi ushirikiano wa nchi kadhaa unaweza kubadilisha tukio hilo kuwa jukwaa la pamoja la utalii, biashara, na kujitangaza kimataifa.
Kombe la Dunia la 2026 halitakumbukwa tu kwa kuvunja rekodi mbalimbali, bali pia kwa uwezo wake wa kuwa hatua muhimu ya mabadiliko katika namna matukio makubwa ya michezo ya kimataifa yanavyopangwa, kutangazwa, na kunufaishwa.
Mwandishi, Daniel Morales Ruvalcaba, ni profesa msaidizi katika Chuo Kikuu cha Sun Yat-sen nchini China na muundaji wa World Power Index X













