Idadi ya maambukizi ya Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo imepita zaidi ya 1,000 huku yakiongezeka kote katika mikoa ya mashariki, kulingana na taarifa za tathmini ya hali iliotolewa na Wizara ya Afya.
Idadi kamili ya maambukizi ya Ebola ni 1,077, huku maambukizi yaliyothibitishwa yakifika 121 na vifo 17 tangu mlipuko huo ulipotangazwa Mei 15.
Wizara imeeleza kuwa Ebola imeathiri maeneo 13 ya kiafya katika mikoa mitatu, ikiwemo Ituri, Kivu Kaskazini, na Kivu Kusini.
“Uchunguzi, vipimo na uhamasishaji wa jamii umeimarishwa licha ya changamoto ya operesheni hiyo kuripotiwa,” ilisema siku ya Jumatano.
Mikusanyiko imepigwa marufuku
Mamlaka za nchini DRC zimepiga marufuku mikusanyiko eneo la Ituri, kitovu cha mlipuko, ikiwemo michezo, ili kuepusha kusambaa kwa Ebola.
Kulingana na Waziri wa Afya Roger Kamba, karibu watu 3,600 wametangamana na wagonjwa.
Mataifa kumi, ikiwemo Rwanda, Kenya, Tanzania, Angola, Burundi, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Jamhuri ya Congo, Ethiopia, Sudan Kusini, na Zambia, yanakabiliwa na hatari ya mlipuko wa Ebola, kulingana na Kituo cha Kupambana na Kudhibiti Magonjwa barani Afrika (Africa CDC).
Maambukizi saba yamerekodiwa kufikia sasa katika nchi jirani ya Uganda tangu mlipuko huu .
Siku ya Jumatano Uganda ilitangaza kufunga kwa muda mpaka wake na DRC ili kupunguza hatari ya kusambaa kwa ugonjwa huo nchini.
Shirika la Afya Duniani (WHO) limeeleza kiwango cha tahadhari “kuwa juu,” na nchi kadhaa jirani ya DRC zimeimarisha hatua za kudhibiti virusi hivyo visisambae, ikiwemo kuweka masharti ya kusafiri kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.


















