Rais wa Iran Masoud Pezeshkian amesema siku ya Alhamisi kuwa mataifa ya Kiislamu yasiruhusu maeneo yao kutumiwa katika kushambulia nchi zingine za Kiislamu.
“Kutetea Iran hakumaanishi uhasama dhidi ya mataifa mengine ya Kiislamu au nchi jirani,” Pezeshkian alisema katika hotuba iliyooneshwa na shirika la habari la taifa la Iran wakati wa Kongamano la Kimataifa la Umoja wa Waislamu jijini Tehran.
“Taifa lolote la Kiislamu lisiruhusu ardhi yake kutumiwa kufanya mashambulizi dhidi ya taifa lingine la Kiislamu. Taifa lolote la Kiislamu lisitafute usalama wake kupitia kukosekana kwa usalama wa majirani zake,” alisema.
Akizungumza kuhusu vita na Marekani, Pezeshkian alisema mashambulizi makubwa ya kijeshi ya Marekani na Israel dhidi ya Iran yalianza wakati juhudi za kidiplomasia zilikuwa zimeanza kati ya Iran na Marekani kusuluhisha tofauti zao.
Alisema mazungumzo ya Iran na Marekani yalianza tena mwezi huo katika jitihada za kutafuta suluhu ya kidiplomasia wakati mashambulizi hayo yalipoanza, na kuwaua makamanda wa Iran, maafisa, wanasayansi, wanafunzi, watoto wa shule na raia, pamoja na kushambulia miji na miundombinu.
Kulingana na shirika la habari la serikali la Iran IRNA, karibu wageni wa ndani ya nchi na wa kimataifa kutoka mataifa 40, ikiwemo Iraq, Pakistan, Uturuki, Lebanon na Afghanistan, wanahudhuria mkutano huo.
Kongamano hilo litaendelea hadi Jumapili, huku kukiwa na hafla katika miji ya Tehran, Qom na Mashhad, pamoja na mikutano minne maalum Magharibi mwa Azerbaijan, Kordestan, Golestan na mikoa ya Razavi Khorasan.























