| Swahili
UTURUKI
4 dk kusoma
Mkutano wa Stratcom 2026 wafunguliwa Istanbul wakati mvutano wa kimataifa ukiongezeka
Viongozi kutoka nchi 38 wamekutana kukabiliana na upotoshaji wa taarifa, simulizi zinazoendeshwa na akili mnemba (AI), na migogoro ya kijiografia inayobadilisha mfumo wa kimataifa, chini ya kaulimbiu ya misukosuko ya kimataifa na kurejesha utulivu.
Mkutano wa Stratcom 2026 wafunguliwa Istanbul wakati mvutano wa kimataifa ukiongezeka
Makamu wa Rais wa Uturuki Cevdet Yilmaz akitoa hotuba wakati wa mkutano wa Stratcom 2026 Machi 27 2026 mjini Istanbul, Uturuki. / / AA
tokea siku moja

Mkutano wa Kimataifa wa Mawasiliano ya Kimkakati (Stratcom Summit) 2026 ulianza siku ya Ijumaa mjini Istanbul, Uturuki ukiwakutanisha maafisa waandamizi kutoka nchi 38 kujadili vita vya Mashariki ya Kati na changamoto pana zinazoikabili mfumo wa kimataifa.

Umeandaliwa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Uturuki, mkutano huo wa siku mbili unaofanyika kuanzia Machi 27 hadi 28 utahudhuriwa na Makamu wa Rais wa Uturuki Cevdet Yilmaz, Waziri wa Mambo ya Nje Hakan Fidan, na Mkurugenzi wa Shirika la Ujasusi la Taifa Ibrahim Kalin.

Mawaziri 11 kutoka nchi 10 watakuwa miongoni mwa zaidi ya maafisa waandamizi 60 wanaoshiriki katika mkutano huo.

Chini ya kaulimbiu “Misukosuko katika Mfumo wa Kimataifa: Migogoro, Simulizi na Utafutaji wa Mpangilio,” mkutano huo utaangazia mabadiliko ya kimuundo katika mfumo wa dunia, migogoro inayotokana nayo, pamoja na mbinu za kikanda za kurejesha utulivu wa kimataifa.

“Binadamu wanahitaji amani, na amani inahitaji haki”

Katika hotuba yake ya ufunguzi kwenye mkutano huo, Makamu wa Rais wa Uturuki Cevdet Yilmaz alionya kuwa kuongezeka kwa ukosefu wa utulivu duniani, vita na upotoshaji wa simulizi kunabadilisha siasa za kimataifa pamoja na kuangazia umuhimu wa mawasiliano ya kimkakati katika uongozi.

Alisema mpangilio wa dunia baada ya Vita vya Pili vya Dunia uko chini ya shinikizo linaloongezeka kadri mizani ya nguvu inavyobadilika kwa kasi kuliko taasisi zinavyoweza kufuatilia, huku migogoro inayogusa usalama, uchumi, tabianchi na uhamiaji ikizidi kuwa sehemu ya kudumu ya siasa za kimataifa.

Yilmaz alitaja vita vinavyohusisha Israel na Marekani dhidi ya Iran kama tishio kubwa kwa utulivu wa kikanda na kimataifa, akiashiria madhara ya kibinadamu na kiuchumi, na kusema Uturuki inajitahidi kufanikisha kusitishwa mara moja kwa mapigano kupitia ushirikiano wa kidiplomasia unaoongozwa na Rais Recep Tayyip Erdogan.

Pia alikosoa vitendo vya Israel huko Gaza, Ukingo wa Magharibi unaokaliwa, Lebanon na Syria, pamoja na vizuizi katika Msikiti wa Al-Aqsa ulioko Jerusalem Mashariki inayokaliwa, akitoa wito kwa jamii ya kimataifa kupinga vikali zaidi wa ukiukwaji wa Israel dhidi ya sheria za kimataifa.

Akionya kuwa migogoro ya kisasa inazidi kuathiriwa na upotoshaji wa taarifa na maudhui yanayotengenezwa na akili mnemba, Yilmaz alisema kuwa vita vya taarifa na vikwazo vya ufikiaji wa vyombo vya habari vinazidi kufanya iwe vigumu kupata taarifa za kuaminika.

Alisisitiza nafasi ya kidiplomasia ya Uturuki, akitaja juhudi za upatanishi kuanzia vita vya Urusi na Ukraine hadi barani Afrika, na kusema Uturuki inasalia kuwa miongoni mwa wachache wanaoweza kuwasiliana na pande zote — za Mashariki na Magharibi.

“Nchi tano haziwezi kuwakilisha dunia nzima… Binadamu wanahitaji amani, na amani inahitaji haki,” alisema Yilmaz, akiongeza: “Tunalenga kuwa wa haki na wenye nguvu.”

Alimalizia kwa kusema kuwa mawasiliano ya kimkakati sasa ni muhimu katika kudhibiti hatari na akatoa wito wa ushirikiano wa karibu zaidi kati ya serikali, vyombo vya habari, wasomi na asasi za kiraia.

“Vitisho haviji kwa risasi bali kwa upotoshaji”

Burhanettin Duran pia alisema kuwa mkutano huo, ambao “umekuwa maarufu kimataifa,” unazidi kuvutia uangalizi mkubwa wa dunia.

“Tutashughulikia masuala ya uaminifu katika uwanja wa mawasiliano ya kimkakati sambamba na ajenda ya kimataifa na kushiriki katika ubadilishanaji mpana wa mawazo,” alisema Duran.

Alisema mkutano huo unafanyika chini ya kaulimbiu “Misukosuko katika Mfumo wa Kimataifa: Migogoro, Simulizi na Kurejesha Mpangilio,” inayodhihirisha hali ya misukosuko ya mazingira ya sasa ya dunia.

“Katika zama tunazoishi, mawasiliano ya kimkakati, maeneo ya migogoro na majanga hayawezi tena kuangaliwa kwa kujitenga,” alisema, akiongeza kuwa taarifa zimebadilika kutoka kuwa njia ya kusambaza ukweli pekee hadi kuwa chombo cha moja kwa moja cha nguvu na ushindani.

“Leo, vitisho vinaingia katika dunia yetu si kwa mizinga bali kwa mitindo mipya, na haviji kwa risasi bali kwa upotoshaji,” alisema Duran, akisisitiza kuwa kulinda ukweli sasa ni muhimu sawa na kulinda mipaka halisi ya nchi katika mfumo mpya wa usalama unaoibuka.

CHANZO:AA