| Swahili
Maoni
AFRIKA
4 dk kusoma
Hasira ya Afrika Kusini imeelekezwa pasipo sahihi; Afrika haitaendelea kubeba maumivu haya milele
Afrika Kusini haiwezi kuendelea kufurahia faida za biashara ya Afrika, uwekezaji wa Afrika, na mshikamano wa Waafrika huku ikiruhusu raia wake kumwaga damu ya Waafrika wenzao. Huo si Uanamajumui. Huo ni unyonyaji.
Hasira ya Afrika Kusini imeelekezwa pasipo sahihi; Afrika haitaendelea kubeba maumivu haya milele
Maandamano dhidi ya chuki dhidi ya wageni, jijini Johannesburg, Afrika Kusini. / / Reuters

Video hizi zinatisha na kuumiza moyo. Mwanamke wa Ghana akiburuzwa kutoka dukani kwake. Mfanyabiashara wa Nigeria akipigwa hadharani mchana kweupe. Raia wa Afrika Kusini wakishangilia huku Waafrika wenzao wakiporwa na kudhalilishwa. Haya si matukio ya mapya. Ni jinamizi linalojirudia ambalo Afrika Kusini imekataa kuamka kutoka ndani yake.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ghana, Samuel Ablakwa, sasa amefanya mazungumzo ya dharura na Ronald Lamola wa Afrika Kusini baada ya video zilizosambaa kuonyesha Waghana wakishambuliwa. Mamlaka za Afrika Kusini zimeonyesha wasiwasi na kuahidi hatua za haraka. Lakini ni mara ngapi tutasikia ahadi zilezile? Ni maisha mangapi ya Waafrika yatapotea kabla “wasiwasi” haujageuka kuwa hatua za kweli?

Niseme wazi: Waafrika Kusini wana malalamiko ya msingi. Ukosefu wa ajira uko juu ya asilimia 32. Pengo la kiuchumi ni miongoni mwa mabaya zaidi duniani. Huduma za msingi zinawafeli mamilioni ya watu kila siku. Lakini kosa ni kuelekeza lawama kwa Waafrika wengine badala ya sera mbovu za ndani na viongozi mafisadi walioliibia taifa kwa miongo kadhaa.

Mwenye duka kutoka Ghana anayeuza mchele Soweto hakusababisha mgogoro wa makazi wa Afrika Kusini. Mwalimu kutoka Zimbabwe huko Limpopo hakuangusha thamani ya pesa ya Afrika Kusini. Muuguzi kutoka Malawi mjini Pretoria hakubuni mfumo mbovu wa umeme. Waafrika hawa si tatizo; wamefanywa kafara na tabaka la kisiasa lililokosa suluhisho.

Huu ndio ukweli ambao makundi yenye chuki dhidi ya wageni nchini Afrika Kusini yanakataa kuukabili: Waafrika si wemye tatizo. Wao ndio wenye suluhisho.

Uchumi wa biashara

Uchumi wa Afrika Kusini umefungamana kwa kina na bara ambalo sasa linaonekana kushambuliwa. Fikiria ukweli huu: Afrika Kusini huuza bidhaa zenye thamani ya zaidi ya R800 bilioni (takribani Dola bilioni 45 za Marekani) kila mwaka kwa mataifa mengine ya Afrika — kuanzia vifaa vya uchimbaji madini hadi bidhaa za viwandani, kemikali hadi mazao ya kilimo. Kama mataifa matano tu ya Afrika yangeamua kulipiza kwa kupiga marufuku bidhaa za Afrika Kusini, Soko la Hisa la Johannesburg lingeporomoka, Thamani ya Rand ingeshuka vibaya, na mamia ya maelfu ya ajira za Waafrika Kusini zingetoweka mara moja. 

Na madhara yasingeishia kwenye bidhaa pekee. Kwa sasa, mamia ya maelfu ya raia wa Afrika Kusini wanaishi, wanafanya kazi, na wanaendelea vizuri kote Afrika — wataalamu Nairobi, wafanyabiashara Accra, wanafunzi Kigali, wamisionari Lilongwe. Kama mataifa ya Afrika yangeamua kuwafukuza kulipiza kisasi kwa mashambulizi dhidi ya raia wao, Afrika Kusini ingekabiliwa ghafla na kurejea kwa watu wake wenyewe wanaohitaji makazi, ajira, huduma za afya, na shule. Uchumi ambao tayari ni dhaifu ungeweza kusambaratika.

Kwa hiyo nawauliza washambuliaji moja kwa moja: Nani hasa ni mzigo sasa?

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ghana, Ablakwa, amethibitisha kuwa ubalozi wa Ghana nchini Afrika Kusini umempata mmoja wa waathiriwa walioonekana kwenye video hizo na unatoa msaada wa kibalozi. Hilo ni jambo jema. Lakini halitoshi. Serikali za Afrika lazima zipite hatua ya diplomasia na kuingia kwenye hatua za pamoja. Mfumo wa Umoja wa Afrika wa kufuatilia chuki dhidi ya wageni lazima uanzishwe ukiwa na mamlaka halisi ya uchunguzi. Nchi wanachama lazima ziandae hatua za pamoja za kiuchumi na kidiplomasia kulinda raia wao.

Afrika Kusini haiwezi kuendelea kufurahia faida za biashara ya Afrika, uwekezaji wa Afrika, na mshikamano wa Waafrika huku ikiruhusu raia wake kumwaga damu ya Waafrika wenzao. Huo si Uanamajumui. Huo ni unyonyaji.

Vitendo viendane na maneno

Natoa wito kwa Rais Ramaphosa na Waziri Lamola kwenda mbali zaidi ya “wasiwasi” na kuchukua “hatua za haraka” — maneno ambayo tumekuwa tukiyasikia kwa zaidi ya muongo mmoja. Wakamateni wahusika. Walipeni fidia waathiriwa. Anzisheni kampeni za elimu ya umma zitakazowafundisha Waafrika Kusini utegemezi wao wa kiuchumi kwa bara hili. Na kama serikali haiwezi kuwalinda raia wa kigeni, basi mataifa ya Afrika lazima yajilinde yenyewe, ikiwa ni pamoja na kuzingatia tahadhari za usafiri, tathmini ya biashara, na hatua za kidiplomasia.

Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA) linawakilisha nguvu ya uchumi yenye thamani ya Dola trilioni 3.4. Lakini mafanikio yake yanategemea imani. Na imani haiwezi kujengwa juu ya makaburi ya wafanyabiashara wa Ghana au wamiliki wa biashara kutoka Nigeria.

Kwa ndugu zangu wa Afrika Kusini: hasira yenu ni ya msingi, lakini imeelekezwa kwa shabaha isiyo sahihi. Adui si raia wa kigeni anayehangaika pamoja nanyi. Adui ni tabaka la viongozi wanaowaweka katika umaskini huku wakiwagawanya kwa misingi ya utaifa wa uongo. Msikubali maumivu yenu kutumiwa kama silaha.

Afrika inaangalia. Na Afrika haitasahau.

Mwandishi, Kennedy Chileshe, ni Mkurugenzi Mtendaji wa Jubilee Leaders Network nchini Zambia

 

CHANZO:TRT Afrika