Ghana imewataka raia wake kutosafiri kwenda Afrika Kusini kama hakuna ulazima wa kufanya hivyo hadi pale watakapofahamishwa kuhusu maelekezo mengine kutokana na kukithiri kwa mashambulizi ya chuki yanayolenga wahamiaji wa Kiafrika.
Katika taarifa, Wizara ya Mambo ya Nje ya Ghana ilisema Jumatatu kuwa makundi yanayojiita kuwa ya vuguvugu dhidi ya wahamiaji Afrika Kusini yamekuwa yakifanya mashambulizi dhidi ya raia wa kigeni wa Afrika, kusababisha majeraha, kupora, biashara kufungwa na mali kupotea.
Wizara imetoa wito kwa raia wa Ghana kuwa makini zaidi katika mipango yao ya safari na kusafiri tu pale palipo na ulazima wa kwenda Afrika Kusini hadi pale hali ya usalama itakapokuwa shwari.
Raia wa Ghana wanaoishi Afrika Kusini wameshauriwa kuwasiliana mara kwa mara na Ubalozi wa Ghana kupata taarifa za usalama na msaada kutoka kwa ubalozi.
Juhudi za kidiplomasia
Wizara inasema serikali ya Ghana imeanzisha juhudi za kidiplomasia na mamlaka za Afrika Kusini kuhusu matukio hayo.
Iliongeza kuwa balozi mdogo wa Afrika Kusini nchini Ghana ameitwa na Wizara ya Mambo ya Nje kutoa ufafanuzi, suala hilo limefikishwa kwa Umoja wa Afrika, na juhudi zinaendelea kusaidia raia wa Ghana na kuwasafirisha iwapo kuna ulazima wa kufanya hivyo.
Ghana pia ilitoa wito kwa serikali ya Afrika Kusini kuhakikisha usalama wa raia wa Afrika wanaoishi nchini humo na kuhakikisha hali ya usalama inarudi kama kawaida.
Vurugu dhidi ya wahamiaji zimeripotiwa katika baadhi ya maeneo nchini Afrika Kusini tangu Aprili, huku biashara zinazomilikiwa na wahamiaji zikishambuliwa na watu kadhaa kujeruhiwa na raia wengine wa kigeni kuondolewa katika maeneo yaliyoathiriwa.
Mwezi uliopita, Ghana iliomba suala hilo lijadiliwe rasmi katika Mkutano wa 8 wa katikati ya mwaka wa Umoja wa Afrika uliopangwa kufanyika El-Alamein nchini Misri kuanzia Juni 24-27.






















