| Swahili
AFRIKA
1 dk kusoma
Sudan yatungua ndege isiyo na rubani katika jimbo la Blue Nile: Wizara ya Ulinzi
Wizara ya Ulinzi inasema imeangusha ndege isiyo na rubani ilitoka katika eneo la Ethiopia; bado hakuna tamko lolote kutoka Addis Ababa.
Sudan yatungua ndege isiyo na rubani katika jimbo la Blue Nile: Wizara ya Ulinzi
Mapigano kati ya jeshi la Sudan na RSF yamesambaa katika maeneo ya Blue Nile , Darfur / َAA

Wizara ya Ulinzi ya Sudan ilisema Jumapili kuwa ilitungua ndege isiyo na rubani ya "kikosi hasimu" katika jimbo la Blue Nile, kusini-mashariki mwa nchi hiyo.

Katika taarifa iliyotolewa kupitia mtandao wa kijamii wa Facebook, wizara hiyo ilisema ndege hiyo ilirushwa kutoka eneo la Ethiopia na ilikuwa ikiruka juu ya jimbo la Blue Nile, karibu na Kurmuk.

Hakukuwa na tamko kutoka kwa mamlaka za Ethiopia.

Mapema mwezi huu, jeshi la Sudan lilisema kuwa lilitungua ndege tatu zisizo na rubani aina ya FH-95 katika jimbo la Kordofan Kaskazini, kusini mwa nchi hiyo.

Mamlaka za Sudan na mashirika ya kutetea haki za binadamu yamelishutumu kundi la wanamgambo la Rapid Support Forces (RSF) kwa kulenga miundombinu ya kiraia.

Kundi hilo kwa kawaida halitoi maoni kuhusu shutuma hizo, likidai kuwa linafanya kazi ya "kuwalinda raia."

Mbali na Blue Nile na Darfur, majimbo matatu ya Kordofan — Kordofan Kaskazini, Magharibi na Kusini — yameshuhudia mapigano kati ya jeshi na RSF tangu tarehe 25 Oktoba 2025.

Sudan imekumbwa na vita kati ya jeshi na RSF tangu Aprili 2023, hali iliyosababisha vifo vya makumi ya maelfu ya watu na kuwafanya takriban watu milioni 13 kuyahama makazi yao, kulingana na makadirio ya Umoja wa Mataifa na mashirika ya kimataifa.

CHANZO:َAA