Wake wa Marais wa Afrika: Zita Oligui Nguema wa Gabon
Mke wa Rais wa Gabon ni ZIta Oligui Nguema / Reuters
Wake wa Marais wa Afrika: Zita Oligui Nguema wa Gabon
Kama Mama wa Taifa, Zita Oligui Nguema anaangazia zaidi katika huduma ya afya, elimu, na kusaidia idadi ya watu walio katika mazingira hatarishi.

Zita Nyangue Oligui Nguema amekuwa Mke wa Rais tangu Agosti 2023 wakati mume wake Brice Clotaire Oligui Nguema alipokuwa Rais wa Mpito wa Gabon.

Baadaye alichaguliwa kuwa Rais wa nne wa Gabon tangu Mei 2025.

Zita alizaliwa Libreville, mwaka 1978, ana Shahada ya Uzamili katika Biolojia ya Mimea na stashahada ya uzamili katika Mafunzo ya Forodha.

Kabla ya kuwa mke wa Rais, alifanya kazi kama mtumishi wa umma.

Alijiunga na Mamlaka ya Ushuru ya Gabon mwaka wa 2006 na aliteuliwa kama Mkaguzi Mkuu katika Ofisi Kuu ya Uwanja wa Ndege wa Libreville mwaka 2007.

Kama Mama wa Taifa, Zita Oligui Nguema anaangazia hasa huduma ya afya, elimu, na kusaidia idadi ya watu walio hatarini kupitia majukwaa kadhaa ya hadhi ya juu.

Anaendesha wakfu unaoitwa "Ma Bannière," ambao unaangazia kusaidia vijana walio katika mazingira magumu, kuwasaidia kuacha uraibu wa dawa za kulevya, na kuboresha ufikiaji wa huduma za afya na elimu.

Pia anafanya kazi kupanua uwezo maalum wa huduma ya afya ya Gabon, kuvunja unyanyapaa wa kijamii kwa wagumba, na kujenga miundombinu ya matibabu katika nyanja kama vile ya saratani, uzazi, na ugonjwa wa sukari.

Zita Oligui Nguema pia anaendesha taasisi inayoitwa "Educating Linda," ambayo inashirikiana kimataifa kusaidia elimu ya sekondari ya wasichana kwa kusambaza vitabu, kutoa ufadhili wa masomo, na kuhimiza kusoma na kuandika kidijitali na kitaaluma kote nchini Gabon.

Pia anashiriki kikamilifu katika majukwaa ya kibara akiwakilisha nchi yake katika hafla tofauti.

Zita anajitahidi kumuunga mkono mume wake anapoongoza nchi ambayo licha ya kuwa kati ya zile zenye Pato la Taifa la juu zaidi kwa kila mtu Afrika, utajiri upo kwa watu wachache na ukosefu wa ajira uko kwa kiasi kikubwa, hasa miongoni mwa vijana.

CHANZO:TRT Swahili