| Swahili
ULIMWENGU
2 dk kusoma
Iran yashambulia uwanja wa ndege wa Kuwait
Mamlaka nchini Kuwait imesitisha usafiri wa ndege baada ya shambulio la ndege isiyo na rubani kuharibu kituo cha abiria na kujeruhi watu kadhaa.
Iran yashambulia uwanja wa ndege wa Kuwait
Moshi waonekana karibu na matangi ya mafuta kwenye uwanja wa ndege wa Kuwait baada shambulio la ndege zisizo na rubani. / Wengine

Iran imeshambulia Uwanja wa Ndege wa Kuwait kutumia ndege zisizo na rubani (droni) na makombora.  Shambulio hilo limesababisha uharibifu katika Kituo cha Abiria cha Terminal 1 pamoja na kujeruhi watu kadhaa, kulingana na jeshi la Kuwait.

Msemaji wa Wizara ya Ulinzi Brigedia Jenerali Saud Abdulaziz Al-Otaibi alisema "idadi ya ndege zisizo na rubani" zililenga Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kuwait, na kusababisha uharibifu mkubwa kwenye kituo cha abiria na kujeruhi watu kadhaa.

Shambulio hilo lililazimu nchi hiyo kusitisha safari zote za ndege, huku ndege zilizokuwa zikielekea nchini humo zikielekezwa kwenye viwanja vingine vya ndege hadi itakapotolewa taarifa nyingine, kwa mujibu wa Mamlaka Kuu ya Usafiri wa Anga ya Kuwait.

Maafisa hawakutoa maelezo mara moja kuhusu ukubwa wa majeraha au wakati shughuli za ndege zinaweza kuanza tena.

Aidha, Jeshi la Kuwait lilieleza kuwa uharibifu uliosababishwa na shambulio hilo ni “mkubwa.”

Shambulio hilo la uwanja wa ndege limekuja saa chache baada ya Iran na Marekani kushambuliana huku kukiwa na juhudi za kidiplomasia za kumaliza mzozo ulioanza Februari.

Jeshi la Marekani limesema lilifanya mashambulizi kwenye kituo cha kijeshi cha Iran baada ya Iran kurusha makombora kuelekea Kuwait na Bahrain siku ya Jumanne.

Matukio ya hivi punde yanaibua wasiwasi mpya kuhusu usalama wa miundombinu muhimu na mitandao ya usafiri wa kiraia katika Ghuba, eneo ambalo tayari limekumbwa na ongezeko la mashambulizi kwa miezi kadhaa na kukatizwa kwa usafiri wa meli na anga.

CHANZO:TRT World and Agencies