Iran imesema kwa mara nyingine tena inafunga njia muhimu ya meli ya Mlango Bahari wa Hormuz siku ya Jumamosi kutokana na mashambulizi ya Israel nchini Lebanon, na kuyataja kuwa ni ukiukaji wa makubaliano yake na Marekani ya kumaliza vita vya Mashariki ya Kati.
Ndege za kivita za Israel zilifanya mashambulio mabaya kusini mwa Lebanon siku ya Jumamosi, saa chache baada ya Marekani kutangaza kusitishwa upya kwa mapigano huko, na kuua takriban watu 28.
Mashambulizi yanayoendelea ya Israel tayari yalikuwa yameathiri mkataba uliotiwa saini na Marekani na Iran wiki hii ili kusitisha vita vya kikanda katika pande zote - ikiwa ni pamoja na Lebanon, ambayo imekuwa hitaji kuu kwa Tehran.
Ikitaja "ukiukwaji wa mkataba" wa Marekani na "ukiukaji wa mara kwa mara wa utawala wa Kizayuni wa usitishaji vita kusini mwa Lebanon", kamandi kuu ya kijeshi ya Iran ilitangaza Jumamosi kwamba "Mlango wa bahari wa Hormuz utafungwa kwa usafiri wa meli."
‘Makubaliano katika hatari '
Kando, wizara ya mambo ya nje ya Iran ilisema kuwa makubaliano yaliyotiwa saini kati ya Iran na Marekani ya kusitisha vita vya Mashariki ya Kati yatakuwa "matatani" isipokuwa masharti yake yatatekelezwa hivi karibuni.
"Upande mwingine lazima uchukue hatua zinazohitajika haraka iwezekanavyo. Vinginevyo, uelewa mzima utakuwa matatizoni," msemaji wa wizara hiyo Esmaeil Baqaei alisema, kwa mujibu wa shirika rasmi la habari la IRNA.
Mlango huo, ambao ni njia muhimu ya usafirishaji wa mafuta na gesi, ulizuiliwa na Iran kwa muda mrefu wa vita, na kusababisha mtikisiko katika masoko ya nishati ya kimataifa.
Iran ilikuwa imekubali kuifungua tena chini ya makubaliano ya awali na Marekani, na usafiri wa meli ulikuwa ukianza kurejea katika siku za hivi karibuni.
Mazungumzo ya kufuatilia makubaliano ya Marekani na Iran yalikuwa yamepangwa nchini Uswizi siku ya Ijumaa, lakini yaliahirishwa kwa muda usiojulikana huku Israel ikianzisha mashambulizi mabaya nchini Lebanon baada ya wanajeshi wake wanne kuuawa katika mapigano.














