Waziri wa Sheria wa Afrika Kusini Mmamoloko Kubayi anasema raia wa Malawi wasio na hati rasmi 5,000 wameondolewa katika nchi hiyo huku mamlaka zikizidisha juhudi za kukabiliana na taharuki inayoletwa na suala la uhamiaji.
Kubayi alitembelea kituo kimoja ambacho kilikuwa na wahamiaji mjini Durban siku ya Jumapili akiwa pamoja na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje Thandi Moraka, Balozi wa Malawi nchini Afrika Kusini Stella Ndau, Na Kaimu Kamishna wa Polisi Puleng Dimpane.
Kituo hicho kinashughulikia suala la raia wa Malawi ambao wanarudi nyumbani.
Wakati wa ziara hiyo, Dimpane alionya kuwa maafisa wa usalama watachukua hatua kali dhidi ya yeyote ambaye anavunja sheria wakati wa maandamano.
Kukabiliana na waandamanaji
Alisema polisi wamekuja na mpango wa kuhakikisha kuna usalama huku taharuki kuhusu uhamiaji ikiongezeka.
Dimpane anasema mamlaka zina uwezo wa kutosha kukabiiana na hali iwapo sheria itakiukwa
"Mipango inaendelea kuhakikisha kuwa sheria inadumishwa. Kama kuna maandamano, kama sheria itavunjwa, tutakuwepo kuhakikisha kuwa tunatekeleza sheria. Kwa hiyo, tunatoa wito wa maandamano ya amani, tunataka watu waheshimu sheria za nchi," alisema.
Serikali ya Afrika Kusini pia imesisitiza dhamira yake ya kuendeleza uhusiano wa kidiplomasia na mataifa ya Afrika wakati wakiendeleza mchakato wa kuwaondosha watu ndani ya nchi yao.
Afrika Kusini imekabiliwa na lawama za kidiplomasia kutoka kwa mataifa kadhaa ambazo raia wake wametatizwa na maandamano yanayowalenga raia wa kigeni.















