| Swahili
Maoni
AFRIKA
5 dk kusoma
Kwa nini malipo ya fidia ya utumwa na ukoloni ni jambo muhimu sana kwa Afrika mwaka 2026
Fidia siyo misaada ya hisani – inahusu uhamisho wa rasilimali za kifedha na kurekebisha mizani ya nguvu. Kuna haja ya kuvunjwa kwa mifumo inayoiadhibu Afrika mara kwa mara.
Kwa nini malipo ya fidia ya utumwa na ukoloni ni jambo muhimu sana kwa Afrika mwaka 2026
AU ilipitisha azimio la kuainisha utumwa na ukoloni kama uhalifu dhidi ya ubinadamu na mauaji ya halaiki wakati wa mkutano wake wa 39. / Wengine / Others
tokea masaa 2

Na Simba Bvundura

Mara nyingi uelewa huja baada ya muda kupita. Ndivyo ilivyokuwa kwa suala la fidia pamoja na mabadiliko makubwa ya kijiografia ya kisiasa mwaka 2025, na pia swali pana la jinsi Afrika inaweza kujitegemea katika kipindi kigumu kama hiki.

Kwa mwaka 2025, Umoja wa Afrika (AU) ulipitisha kaulimbiu: “Haki kwa Waafrika na Watu wenye Asili ya Kiafrika kupitia Fidia.” Kisha mwezi Julai wa mwaka huo, AU iliimarisha dhamira hiyo kwa kutangaza kipindi cha 2026–2036 kuwa Muongo wa Fidia. Lakini hii ina maana gani?

Fidia, kwa ufafanuzi mpana, na kama ilivyoelezwa kwa ustadi katika dhana ya “malipo makubwa ya kurejesha haki” (the Big payback) , zinajumuisha kuomba msamaha, kulipa fidia, kurekebisha madhara, kuponya majeraha na kurejesha haki kwa dhuluma za kimfumo. Haki ya kweli ya fidia inahitaji mabadiliko ya nguvu—si misaada ya hisani bali mageuzi makubwa ya kiuchumi na kisiasa.

Udhaifu wa mfumo wa sasa wa ushirikiano wa kimataifa—na hivyo haja ya kuuchunguza na kuubadili kupitia mtazamo wa fidia—unaonekana wazi katika maeneo makuu matatu:

Kwanza, mfumo wa kifedha wa kimataifa. Taasisi za Bretton Woods (Benki ya Dunia na IMF) zilianzishwa mwaka 1945 zikiwa na wanachama wanne tu kutoka Afrika: Ethiopia, Liberia, Afrika Kusini na Misri.

Pengo la ufadhili

Iliundwa kwa ajili ya dunia ya baada ya vita, lakini haifai tena kwa karne ya 21. Mifumo yao, hasa uchambuzi wa uhimilivu wa madeni, inaendeleza taswira za hatari ambazo baadaye huonekana katika masoko kama vile tathmini za mikopo, bima na utoaji wa hati fungani.

Aidha, mahitaji ya kila mwaka ya Afrika kwa ajili ya miundombinu yako kati ya dola za Marekani bilioni 130 hadi 170, lakini taasisi hizi zimeshindwa kuziba pengo hilo, licha ya nchi za Afrika kuziendea IMF na Benki ya Dunia jumla ya mara 7,596 tangu mwaka 1945.

Misaada mara nyingi imetolewa kwa mtazamo wa kibabe, ikidumisha utegemezi wa bidhaa za nje, uongozi unaolazimishwa kutoka nje, na mageuzi yasiyo na manufaa.

Zaidi ya hayo, ugawaji wa Haki Maalum za Utoaji (SDRs) uliamuliwa bila ushiriki wa nchi za Afrika, jambo lililozidisha ukosefu wa usawa. Kwa kuwa SDRs hugawiwa kwa mfumo wa mgao, nchi tajiri hupata zaidi kiotomatiki.

Pili, sheria za biashara. Shirika la Biashara Duniani (WTO) lilizinduliwa kwa kuzingatia uchumi wa nchi tajiri, na kuiacha Afrika ikitegemea kuuza bidhaa zenye thamani ndogo huku ikinunua bidhaa zilizotengenezwa kutoka nje.

Vikwazo vya kibiashara vinaendelea kuzuia ushiriki wa haki wa Afrika, na bila mageuzi ya maana, kuna hatari ya kutengwa kabisa katika biashara ya kimataifa.

Tatu, uwakilishi katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa. Kutengwa kwa Afrika kumeanza mwaka 1945, na hadi leo bara hilo halina kiti cha kudumu licha ya kuwa mhusika katika zaidi ya 70% ya maazimio ya Baraza hilo.

Makubaliano ya Ezulwini

Ili kushughulikia hali hii, AU ilipitisha Makubaliano ya Ezulwini mwaka 2005, yakitaka angalau viti viwili vya kudumu vyenye haki ya kura ya turufu na viti vitano visivyo vya kudumu.

Ingawa nchi zenye kura ya turufu zimeonyesha kuunga mkono uwakilishi wa kudumu wa Afrika, mara nyingi msaada huo haujumuishi haki ya turufu.

Kwa msingi huu, viongozi na wananchi wa Afrika wanapaswa kushughulikiaje suala la fidia?

Mkutano wa Fidia wa Accra wa mwaka 2023 uliunda Kamati ya Wataalamu na Kikundi cha Marejeo ya Kisheria chini ya Rais wa zamani wa Ghana, John Mahama.

Wajibu wao ni kupima hasara za kiuchumi zilizosababishwa na dhuluma za kihistoria, na kutoa mfumo wa kisheria unaoweza kutumika kudai fidia.

Ripoti ya hivi karibuni ilibainisha njia mbalimbali za ufadhili, ambapo ushuru wa miamala ya kifedha umeonekana kuwa njia inayowezekana zaidi—ingawa njia nyingine kama malipo ya muda mrefu ya serikali pia zinapaswa kuzingatiwa.

Ikiwa fidia zitachukuliwa kuwa zimefanikiwa, haitoshi kudai malipo ya kifedha pekee. Nchi za Afrika lazima zithibitishe uwezo wao wa kujitegemea ili kubadilisha mfumo wa kimataifa.

Kwa hivyo, AU imeweka Msimamo wa Pamoja wa Afrika kuhusu Fidia, unaotaka kurejeshwa kwa mali, usawa wa elimu, urejeshaji wa utamaduni, na mfumo wa dunia ulio sawa zaidi.

Mwelekeo wa sasa wa dunia unaongeza uharaka wa ajenda hii. Kurudi kwa sera za kujilinda kiuchumi kama “America First” na ushuru mkubwa vinaonyesha kuwa nchi za Amerika Kaskazini na Ulaya zinajifungia ndani.

Hatua za vitendo

Kwanza, viongozi, watunga sera, na sekta binafsi wanapaswa kuchunguza kama maamuzi yao yanayohusisha washirika wa kigeni yanaimarisha au kudhoofisha uhuru wa nchi. Hiki ndicho kipimo cha msingi.

Ingawa baadhi ya viongozi tayari wanafanya hivyo—kama Zimbabwe ilivyokataa mpango wa afya wa Marekani wenye thamani ya dola milioni 376 kwa sababu ya masuala ya uhuru—hatua hizi zinapaswa kuwa za kawaida.

Pili, wahusika hawa wanapaswa kudai haki zao mara kwa mara—usipodai, hupati. Ushirikiano wa nchi za zinanzoendelea unatoa mifano mizuri. Kwa mfano, China ilikuwa nchi ya kwanza isiyo ya Afrika katika kundi la G20 kutambua AfCFTA kupitia mpango wake wa kutotoza ushuru.

Hii inaweka kiwango kipya kwa kuacha mifumo ya zamani ya Bretton Woods, kuheshimu umoja wa kiuchumi wa Afrika, na kutoa mfano wa ushirikiano unaozingatia uhuru.

Mwisho, wadau wanapaswa kushirikiana, kwa mfano kupitia jukwaa kama klabu ya wakopaji ya Afrika. Kwa kupata mikopo ya pamoja kutoka nje na kutumia ukuaji wao wa pamoja kama dhamana, wanaweza kubadilishana mawazo na kuongeza faida zao katika mfumo wa kifedha wa dunia.

Fidia si misaada ya hisani—inahusu uhamisho wa rasilimali na kurekebisha nguvu. Inahitaji kuvunjwa kwa mifumo inayoiadhibu Afrika kila wakati.

Kwa kutangaza Muongo wa Fidia, viongozi wa Afrika wanaonyesha kuwa haki ya fidia itakuwa sehemu ya kudumu ya diplomasia yao.

Ili maono haya yatimie, ni muhimu kuhakikisha kuwa maneno yanageuzwa kuwa vitendo—na kwamba hatua tatu zilizotajwa: kuweka viwango, kudai haki, na kushirikiana, zinakuwa sehemu ya utendaji wa kila siku.

Mwandishi, Simba Bvundura, ni mwanafunzi wa mawasiliano katika shirika la Development Reimagined.

Maoni ya mwandishi hayaakisi misimamo au sera za uhariri za TRT Afrika.

CHANZO:TRT Afrika