Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa, amesema kwamba “watu wanaotafuta kujinufaisha” walipanga mashambulizi dhidi ya wahamiaji huku akijaribu kuzituliza nchi nyingine za Afrika ambazo zimeonyesha wasiwasi kuhusu raia wao.
“Ni lazima tuweke wazi kwamba hakuna nafasi ya chuki dhidi ya wageni, uchochezi wa kikabila, kutostahmiliana au vurugu nchini Afrika Kusini,” Ramaphosa alisema katika taarifa iliyotolewa na ofisi yake Jumatatu wakati mjadala kuhusu suala hilo ukiendelea kushika kasi.
Mfululizo wa maandamano dhidi ya wahamiaji katika wiki za hivi karibuni kote Afrika Kusini, pamoja na kuwepo kwa madai ya mashambulizi dhidi ya wageni, ulisababisha Nigeria na Ghana kueleza wasiwasi wao.
Nigeria ilisema wiki iliyopita kwamba itawarudisha nyumbani raia wake 130.
“Maandamano ya hivi karibuni yenye vurugu na vitendo vya kihalifu vilivyolenga raia wa kigeni katika baadhi ya maeneo ya nchi yetu haviwakilishi maoni ya watu wa Afrika Kusini wala sera ya serikali yetu,” alisema Ramaphosa.
“Haya ni matendo ya watu wanaotafuta kujinufaisha kwa kutumia malalamiko halali, hasa ya watu maskini, kwa kujificha chini ya mwavuli wa uongo wa ‘uanaharakati wa kijamii’,” aliandika.
Maandamano dhidi ya wahamiaji
Mamia kadhaa ya watu walishiriki katika moja ya maandamano ya hivi karibuni wiki iliyopita mjini Durban, wakidai hatua zichukuliwe dhidi ya wahamiaji wasiokuwa na nyaraka halali.
Maandamano mengine yamedai kwamba raia wa kigeni wanyimwe huduma za afya.
Mvutano wa kisiasa umeongezeka nchini Afrika Kusini huku kampeni za uchaguzi wa serikali za mitaa wa Novemba zikiongezeka.
Ramaphosa alisema kwamba Afrika Kusini “Lazima ishughulikie kwa uthabiti… na kwa mujibu wa sheria… changamoto ya uhamiaji haramu, ambao unatishia uthabiti wetu wa kijamii, utawala na usalama wa taifa.”
“Wahamiaji wasio na nyaraka halali unaongeza mzigo katika huduma za afya, makazi na huduma za manispaa, hasa katika jamii maskini,” aliongeza, huku akiwashutumu baadhi ya waajiri kwa “kuwatumia vibaya wafanyakazi wa kigeni wasio na nyaraka ambao ni wa gharama nafuu badala ya kuajiri raia na kuwalipa mishahara halali.”
Nigeria ilisema wiki iliyopita kwamba itaandaa safari za dharura za kuwarejesha nyumbani raia wake, ilimwita balozi wa Afrika Kusini mjini Abuja na kutaka uchunguzi ufanyike kuhusu vifo vya Wanigeria wawili katika matukio yaliyohusisha maafisa wa usalama wa Afrika Kusini mwezi uliopita.
Ghana pia ilimwita balozi wa Afrika Kusini mwezi uliopita kupinga “vitendo vya chuki dhidi ya wageni.”
















