Umoja wa Ulaya umeweka vikwazo vipya vinavyolenga biashara ya dhahabu ya Sudan katika juhudi za kuzuia chanzo kikubwa cha ufadhili kwa mgogoro wa zaidi ya miaka mitatu nchini humo kati ya Vikosi vya Jeshi la Sudan (SAF) na Vikosi vya Usaidizi wa Haraka vya Kijeshi (RSF).
Hatua mpya zinapiga marufuku ununuzi, uagizaji au uhamisho wa dhahabu inayotoka Sudan hadi EU. Pia zinakataza uuzaji, usambazaji, uhamisho au usafirishaji wa zebaki na sianidi kwenda Sudan, kemikali mbili zinazotumika sana katika uchimbaji wa dhahabu.
EU ilisema vikwazo hivyo vinalenga kuvuruga uchumi wa vita huku vikipunguza uwezo wa vikundi vyenye silaha kufaidika na utajiri wa madini wa nchi hiyo.
Baraza la Umoja wa Ulaya lilisema vikwazo hivyo vimeundwa "kupunguza vyanzo vya ufadhili wa mgogoro" na kuongeza shinikizo kwa wale wanaochochea vita.
Hata hivyo ruhusa itatolewa kwa madini ya zebaki na sianidi wakati vifaa hivyo vinakusudiwa kwa ajili ya misaada ya dharura, afya ya umma au kukabiliana na maafa.
Dhahabu ni mojawapo ya bidhaa za thamani zaidi za mauzo ya nje za Sudan na imekuwa chanzo muhimu cha mapato kwa pande zote mbili katika mzozo huo. Wachambuzi na waangalizi wa kimataifa wameonya mara kwa mara kwamba udhibiti wa migodi ya dhahabu na mitandao ya magendo umesaidia kuendeleza mapigano licha ya kuongezeka kwa vikwazo vya kimataifa.
Mgogoro huo uligeuka kuwa vita kamili mwezi Aprili 2023 baada ya RSF kuanzisha mashambulizi dhidi ya vituo vya kijeshi, jambo lililosababisha mapigano na Jeshi la Sudan linaloongozwa na Jenerali Abdel Fattah al-Burhan. Mzozo huo umesababisha moja ya migogoro mibaya zaidi ya kibinadamu duniani, na kuwafanya mamilioni ya watu kuhama makazi yao na kuharibu sehemu kubwa za nchi.
Hatua za hivi karibuni zinapanua mfumo wa vikwazo wa EU uliopo dhidi ya Sudan, ambao tayari umewalenga viongozi wa kijeshi, makampuni na vyombo vinavyoshutumiwa kudhoofisha utulivu wa nchi na mpito wa kisiasa.













