Afrika Kusini imeelekea kwenye kambi yake ya mazoezi ya Kombe la Dunia Pachuca siku ya Jumatatu kabla ya mechi yao dhidi ya wenyeji Mexico Juni 11, lakini bila kocha msaidizi Helman Mkhalele ambaye hajapata viza ya Marekani.
Ndege ya kukodi iliondoka jijini Johannesburg baada ya saa 24 za hekaheka ambapo awali walitarajiwa kuondoka siku ya Jumapili, lakini haikuwezekana kutokana na kucheleweshwa kwa viza kwa kile kilichoelezwa kuwa tatizo la usimamizi kwa Shirikisho la Soka la Afrika Kusini (SAFA).
Mkhalele, winga wa zamani wa kimataifa ambaye alicheza katika timu ya taifa ya Bafana Bafana mara 66, ikiwemo mara ya kwanza katika Kombe la Dunia Ufaransa 1998, itabidi kuungana na timu baadaye kutokana na kunyimwa viza hapo awali.
"Wametunyima viza (Ubalozi Mdogo wa Marekani Johannesburg), lakini hawakutoa ufafanuzi. Ni tatizo kubwa kukabiliana na hali hii ambapo haupati taarifa yoyote," rais wa SAFA Danny Jordaan aliliambia Shirika la Habari la Taifa la Serikali siku ya Jumatatu.
'Hatufahamu chochote'
"Hatujui kwa nini (walimnyima viza), hatufahamu chochote, lakini tuna matumaini kuwa suala hilo litatatuliwa (karibuni). Wachezaji wote wako (ndani ya ndege) na asilimia 99 ya benchi la ufundi."
Afrika Kusini inacheza na Jamaica mechi ya kirafiki siku ya Ijumaa kabla ya kukabiliana na Mexico kwenye mechi ya Kombe la Dunia katika mji wa Mexico City.
Mara ya nne kwa Afrika Kusini
Afrika Kusini iko kwenye kundi A na itacheza na Jamhuri ya Czech huko Atlanta Juni 18 na Korea Kusini mjini Monterrey, Mexico siku sita baadaye.
Hii ni mara yao ya nne kucheza katika fainali za Kombe la Dunia na wana matumaini kuwa watapita hatua za makundi kwa mara ya kwanza.














