| Swahili
AFRIKA
2 dk kusoma
Mchekeshaji wa Kenya Eric Omondi akamatwa kwa maandamano kupinga kupanda bei ya mafuta
Mawakili wa Omondi walidai wapelelezi walikataa kumwachilia mwanaharakati huyo kwa dhamana na kutaja mashtaka kuwa "ya kipuuzi."
Mchekeshaji wa Kenya Eric Omondi akamatwa kwa maandamano kupinga kupanda bei ya mafuta
DCI imesema washukiwa wengine kadhaa wanaohusishwa na visa hivyo tayari wamekamatwa na kufikishwa mahakamani. / Reuters

Kukamatwa kwa mchekeshaji aliyegeuka kuwa mwanaharakati wa Kenya Eric Omondi kumezua wimbi jipya la ukosoaji kutoka kwa wanasiasa wa upinzani na mashirika ya kiraia waliotaka aachiliwe mara moja.

Omondi alikamatwa Ijumaa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) na maafisa kutoka Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI), ambao walisema mwanaharakati huyo anachunguzwa kuhusu makosa yanayodaiwa kufanywa wakati wa maandamano ya hivi majuzi ya bei ya mafuta jijini Nairobi.

Kulingana na DCI, kukamatwa huko kulifuatia kile ilichotaja kama ujasusi wa kuaminika unaomhusisha Omondi na uhalifu unaotekelezwa chini ya kivuli cha maandamano.

"Kufuatia upelelezi wa kuaminika, wapelelezi kutoka DCI ya Kati, wanaofanya kazi kwa pamoja na CRIB Mkoa wa Nairobi, walimkamata mshukiwa kuhusiana na makosa yaliyofanywa kwa kisingizio cha maandamano ya hivi majuzi yanayohusiana na mafuta jijini Nairobi. Kwa sasa anarekodi taarifa yake katika Makao Makuu ya DCI ya Kanda ya Nairobi alipokuwa akishughulikiwa ili afikishwe mahakamani," ilisema taarifa hiyo iliyotumwa na DCI kwenye ukurasa wao wa X.

Maandamano hayo yalizuka baada ya ongezeko kubwa la bei ya mafuta kuzua hasira za wananchi na kutatiza usafiri kote nchini.

Omondi alikua mmoja wa watu wanaoonekana zaidi katika maandamano hayo, na kufanya maandamano ya hadhi ya juu katika wilaya ya kati ya biashara ya Nairobi, ikiwa ni pamoja na vitendo vya kiishara vya kutupa mamia ya mitungi kwenye mitaa ya Nairobi kupinga ongezeko kubwa la bei ya mafuta.

Miongoni mwa hisia kali kuhusu kukamatwa kwake zilitoka kwa Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, ambaye alimtembelea Omondi katika makao makuu ya DCI na kukosoa uamuzi wa kumweka kizuizini.

Owino, ambaye ni sehemu ya timu ya wanasheria wa Omondi, alidai wachunguzi walikataa kumwachilia mwanaharakati huyo kwa dhamana na kutaja mashtaka kuwa "ya kipuuzi."
Alitoa wito kwa wafuasi kufuata taratibu za mahakama Omondi atakapofikishwa mbele ya hakimu.

DCI imetetea hatua yake, ikisisitiza kuwa ingawa Wakenya wamehakikishiwa haki ya kukusanyika na kuandamana kwa amani, vitendo vya uhalifu vilivyotendwa wakati wa maandamano vitachunguzwa na kufunguliwa mashtaka. Shirika hilo limesema washukiwa wengine kadhaa wanaohusishwa na visa hivyo tayari wamekamatwa na kufikishwa mahakamani.

Omondi atafikishwa kortini Jumatatu Juni 8.


CHANZO:TRT Afrika Swahili