| Swahili
UTURUKI
2 dk kusoma
Uturuki itaendelea kuwa chanzo cha matumaini kwa Gaza na dunia: Erdogan
Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan, amesema nchi yake itaendelea kuwasaidia watu wenye mahitaji duniani kote, hususan huko Gaza, na kutoa matumaini kwa waathiriwa wa migogoro na hali ngumu za maisha.
Uturuki itaendelea kuwa chanzo cha matumaini kwa Gaza na dunia: Erdogan
"Tutaendelea kuwaunga mkono watu wenye uhitaji katika sehemu nyingi duniani, hasa Gaza," alisema Erdogan. / / AA

Uturuki itaendelea kuwasaidia watu wenye mahitaji duniani kote, hususan huko Gaza, na kutoa matumaini kwa waathiriwa wa migogoro na hali ngumu za maisha, amesema Rais wa nchi hiyo, Recep Tayyip Erdogan.

Katika ujumbe wake wa kuadhimisha Siku ya Misaada ya Kibinadamu Duniani, Erdogan amesema Uturuki inaendelea kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza katika utoaji wa misaada ya kibinadamu, akisisitiza kuwa msimamo huo unatokana na historia ya nchi hiyo pamoja na maadili yake ya muda mrefu ya ustaarabu.

“Leo ni Siku ya Misaada ya Kibinadamu Duniani. Kutokana na ujasiri wa historia yetu na maadili ya ustaarabu wetu wa kale, tunaendelea kuwa mfano kwa kila mtu katika suala hili linalovuka mipaka ya siasa, na kubaki kuwa nchi inayotoa misaada mingi zaidi ya kibinadamu duniani ikilinganishwa na pato lake la taifa,” Erdogan amesema kupitia mtandao wa kijamii wa Uturuki, NSosyal.

Amesema kwamba suala la kuwa zaidi ya watu milioni 300 hawana mahitaji ya msingi na wanahangaika kuishi katika mazingira magumu unapaswa kuwa wito kwa jumuiya ya kimataifa kuwajibika.

“Tutaendelea kusimama pamoja na watu wenye mahitaji”

Erdogan amesema kuwasaidia wanaodhulumiwa, mayatima, wanyonge na wenye mahitaji, pamoja na kuwa karibu na wale ambao hawana wa kuwasaidia, ni sehemu ya mafundisho ya dini.

“Uturuki itaendelea kunyoosha mkono wake wa huruma popote ambapo kuna mtu mwenye mahitaji. Tutaendelea kusimama pamoja na watu wenye mahitaji katika maeneo mbalimbali duniani, hasa Gaza, na kuwa chanzo cha matumaini kwa wanaodhulumiwa na waathiriwa,” alisema.

Kauli hiyo imekuja wakati Gaza ikiendelea kukabiliwa na madhara makubwa ya kibinadamu yaliyosababishwa na vita vya Israel katika eneo hilo lililozingirwa.

Kwa mujibu wa Wizara ya Afya ya Palestina, idadi ya watu waliouawa tangu Israel kuanza mashambulizi yake Gaza mwezi Oktoba 2023 imefikia 73,407, huku wengine 174,335 wakijeruhiwa.

Wizara hiyo ilisema kuwa tangu makubaliano ya kusitishwa kwa mapigano kuanza kutekelezwa, Wapalestina 1,273 wameuawa na wengine 4,223 wamejeruhiwa katika ukiukaji wa makubaliano unaofanywa na Israel.

Mbali na vifo na majeruhi, mashambulizi ya Israel yamesababisha uharibifu mkubwa katika Gaza, huku takribani asilimia 90 ya miundombinu ya kiraia ikiharibiwa. Umoja wa Mataifa umekadiria gharama za kuijenga upya Gaza kuwa karibu Dola bilioni 70.