Timu ya taifa ya soka ya Afrika Kusini, maarufu Bafana Bafana, itaondoka kuelekea kushiriki katika michuano ya Kombe la Dunia 2026 huko Amerika Kaskazini siku ya Jumatatu baada ya tatizo la ucheleweshaji wa viza, ambalo lilitishia kuvuruga mipango ya safari ya timu, kutatuliwa kwa kiasi kikubwa.
Timu hiyo ilitarajiwa kuondoka kuelekea Mexico mapema Jumapili, lakini sasa itaondoka baada ya zaidi ya saa 24.
Hata hivyo wajumbe wanne wa msafara huo bado wanasubiri viza zao: kocha msaidizi, daktari wa timu, mkuu wa usalama na mchambuzi mmoja wa timu.
Hapo awali Waziri wa Michezo wa Afrika Kusini, Gayton McKenzie, alikuwa amelikosoa Shirikisho la Soka la Afrika Kusini (SAFA) kwa matatizo ya usimamizi yaliyosababisha ucheleweshaji huo, alithibitisha kuwa wachezaji wote wamepokea nyaraka zao za kusafiria.
Wasiwasi kuhusu visa
“Wachezaji wote wa Bafana Bafana wamepokea visa zao za kusafiria kwenda Marekani. Wanaosalia ni kocha msaidizi, daktari wa timu, mkuu wa usalama na mchambuzi mmoja,” McKenzie aliandika kwenye mtandao wa kijamii wa X.
“Ndege itaondoka Jumatatu,” aliongeza.
Kuchelewa kwa visa kulizua wasiwasi kuhusu maandalizi ya timu kwa mashindano hayo, ambayo yataandaliwa kwa pamoja na Marekani, Mexico na Canada.
Bafana Bafana wanatarajiwa kucheza mechi ya kirafiki dhidi ya Jamaica nchini Mexico kama sehemu ya maandalizi kabla ya kuanza kwa michuano.
Baadaye, Afrika Kusini itaanza kampeni yake ya Kombe la Dunia kwa kucheza dhidi ya wenyeji wenza, Mexico, katika Mexico City tarehe 11 Juni.














