| Swahili
AFRIKA
2 dk kusoma
Watu 20,000 walazimika kuhama makazi yao kutokana na mapigano Blue Nile Sudan
Kundi la ndani la misaada na kushughulikia dharura lilihimiza mashirika ya kibinadamu na ya kutoa misaada, pamoja na taasisi za ndani na za kimataifa, kuingilia kati kwa dharura.
Watu 20,000 walazimika kuhama makazi yao kutokana na mapigano Blue Nile Sudan
Sudan imekumbwa na vita kati ya jeshi na RSF tangu mwezi wa Aprili 2023. / َAA

Takriban watu 20,000 wamelazimika kuhama makazi yao katika jimbo la Blue Nile nchini Sudan kutokana na kuzorota kwa hali ya usalama na kuongezeka kwa hatari zinazowakabili wakazi, kulingana na kundi la ndani la kutoa misaada siku ya Jumapili.

Katika taarifa yake, Kundi la Kushughulikia Dharura la Geissan (Geissan Emergency Room) lilisema kuwa eneo la City 12 katika wilaya ya Geissan linashuhudia wimbi jipya la watu kuhama makazi yao, likiwemo kundi la wakazi pamoja na raia waliokuwa wakihifadhiwa katika vituo vya muda.

Makadirio ya awali yanaonyesha kuwa "idadi ya watu waliokimbia makazi yao inakaribia 20,000, wakiwemo familia, watoto, wanawake na wazee," taarifa hiyo iliongeza.

Watu hao waliokimbia makazi yao wametawanyika katika maeneo kadhaa, ikiwemo Shira, Abu Qami na Al-Hilla Al-Qadima, pamoja na wilaya ya Wad Al-Mahi iliyo upande wa mashariki, huku wengine wakielekea kwenye vituo vya hifadhi katika mji wa Damazin, kundi hilo lilisema.

Madhara ya kibinadamu

Kundi hilo lilibainisha kuwa familia zilizokimbia makazi zinakabiliwa na "hali mbaya ya kibinadamu" huku kukiwa na uhaba mkubwa wa vifaa vya kujenga makazi na mahitaji muhimu ya msingi.

Kundi hilo la dharura lilihimiza mashirika ya kibinadamu na ya kutoa misaada, pamoja na taasisi za ndani na kimataifa, kuingilia kati kwa haraka ili kukidhi mahitaji yanayoongezeka ya watu hao na kusaidia kupunguza madhara ya kibinadamu na kiafya yanayotokana na mgogoro huo.

Jimbo la Blue Nile limeshuhudia kuongezeka kwa mapigano katika siku mbili zilizopita kufuatia mashambulizi yaliyofanywa na kundi la wanamgambo la Rapid Support Forces (RSF) na washirika wao wa Sudan People’s Liberation Movement-North (SPLM-N) katika maeneo kadhaa ya jimbo hilo.

Mbali na Blue Nile na Darfur, majimbo matatu ya eneo la Kordofan — Kordofan Kaskazini, Magharibi na Kusini — yameshuhudia mapigano kati ya jeshi na RSF tangu tarehe 25 Oktoba.

Sudan imekuwa ikikabiliwa na vita kati ya jeshi na RSF tangu mwezi Aprili 2023, vita ambavyo vimesababisha vifo vya makumi ya maelfu ya watu na kuwafanya takriban watu milioni 13 kuyahama makazi yao, kulingana na makadirio ya Umoja wa Mataifa na mashirika ya kimataifa.

CHANZO:َAA