Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Afrika cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (Africa CDC) ametoa wito wa kuchukuliwa hatua za dharura kudhibiti mlipuko wa Ebola unaoendelea kuongezeka katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Ameonya kuwa ikiwa hatua za kuzuia virusi hivyo hazitachukuliwa mara moja, mlipuko huo unaweza kuwa mbaya zaidi kuwahi kushuhudiwa duniani.
Siku 65 tangu mlipuko huo utangazwe rasmi mnamo Mei 15, idadi ya maambukizi iliyothibitishwa imefikia 2,423 kufikia Jumanne, ikiwemo vifo 967, kulingana na taarifa ya Wizara ya Afya.
Kiwango cha vifo kutokana na ugonjwa huo kimefikia asilimia 39.9, huku kiwango cha ufuatiliaji wa watu waliokutana na wagonjwa kikiwa asilimia 81.1.
"Mlipuko wa Ebola unaongezeka kwa kasi ya kutisha. Ni lazima tuchukue hatua sasa. Tusipovidhibiti virusi hivi leo, huu utakuwa mlipuko mbaya zaidi kuwahi kurekodiwa duniani," alisema Jean Kaseya, Mkurugenzi Mkuu wa Africa CDC, kupitia ujumbe aliouchapisha kwenye mtandao wa kijamii wa X.
Aliongeza kuwa: "Huu si wakati wa kuchelewa. Lazima tuhamasishe rasilimali zote zilizopo, tuimarishe juhudi za kukabiliana na mlipuko huu katika maeneo yaliyoathirika, na tuukomeshe kabla haujasababisha vifo zaidi."
Virusi hivyo vimeathiri majimbo matano ambayo ni Haut-Uele, Ituri, North Kivu, South Kivu na Tshopo.
Jimbo la Ituri linaendelea kuwa kitovu cha mlipuko huo unaosababishwa na aina ya virusi vya Bundibugyo, ambapo maambukizi yanaendelea kusambaa.
Kaseya alisisitiza kuwa ni muhimu kukumbuka kwamba nyuma ya kila takwimu kuna binadamu, familia na jamii inayopitia madhara ya ugonjwa huo.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), idadi ya maeneo ya afya yaliyoathirika imeongezeka kutoka 36 hadi 42 katika kipindi cha wiki moja iliyopita.












