Hakan Fidan amesema kuwa kufanikisha amani katika vita kati ya Urusi na Ukraine ni jambo la msingi kwa utulivu na usalama wa eneo hilo, huku akisisitiza umuhimu unaokua wa ushirikiano wa kimkakati kati ya Uturuki, Azerbaijan na Georgia.
“Vita vinavyoendelea kaskazini mwetu vinaathiri moja kwa moja usalama wa eneo letu. Tunaona kuwa kufanikisha amani katika vita vya Urusi na Ukraine ni muhimu kwa utulivu na usalama wa eneo letu. Tunaamini mchakato huu wa kidiplomasia na juhudi za amani lazima ziendelee kwa uamuzi na uthabiti,” Fidan amesema siku ya Jumatatu.
Waziri huyo alizungumza katika mkutano wa pamoja na waandishi wa habari baada ya Mkutano wa 10 wa Mawaziri wa Mambo ya Nje wa pande tatu kati ya Uturuki, Azerbaijan na Georgia uliofanyika katika Kasri ya Çırağan mjini Istanbul, pamoja na mawaziri wenzake Jeyhun Bayramov (Azerbaijan) na Maka Botchorishvili (Georgia).
“Sote tunafuatilia kwa wasiwasi mkwamo uliopo sasa katika uwanja wa vita na katika mchakato wa kidiplomasia. Hatua zinazochukuliwa na pande husika kujaribu kutumia mkwamo huu kwa faida yao, kwa bahati mbaya zinaongeza zaidi mvutano katika eneo la mapigano.”
Akizungumzia mashambulizi ya hivi karibuni katika Bahari Nyeusi na Bahari ya Azov, Fidan alisema yanaonyesha madhara makubwa yanayoweza kutokana na mzozo huo, na akatoa rambirambi kwa Azerbaijan kufuatia tukio la hivi karibuni lililosababisha vifo.
Matarajio ya matokeo ya mkutano
Fidan alisema kuwa utaratibu wa ushirikiano wa pande tatu umebadilika na kuwa jukwaa linalozingatia matokeo ambalo linaimarisha uaminifu katika eneo hilo.
“Leo tunafanya mkutano wa kumi wa utaratibu wa pande tatu tuliouanzisha kwa hisia ya watu wa kanda hili. Mkutano wetu umeonesha tena kuwa mfumo huu umekuwa jukwaa la mashauriano linalozalisha matokeo na kujenga imani katika eneo letu.”
Ameongeza kuwa utaratibu huo, ambao umekuwa ukiendelea bila kukatika kwa takribani miaka 14, umechangia katika mazungumzo ya kisiasa, ushirikiano wa kiuchumi, usafirishaji, usalama wa nishati, biashara na kuimarisha uhusiano wa watu kwa watu.
“Tunaona mfumo huu si tu kama unaohudumia maslahi ya pamoja ya nchi zetu tatu, bali pia kama moja ya nguzo za amani, utulivu na ustawi endelevu katika eneo la Caucasus Kusini.”
Usalama wa nishati na Njia ya Kati (Middle Corridor) vimeangaziwa
Fidan amesisitiza kuwa mvutano wa kijiopolitiki, hali ya kutokuwa na uhakika wa kiuchumi, na wasiwasi unaoongezeka kuhusu usalama wa nishati umeongeza thamani ya ushirikiano wa kikanda.
Amesema: “Katika kipindi kama hiki, mazingira ya amani na ushirikiano tuliyoyajenga katika eneo letu yana thamani halisi ya kimkakati.”
Ameeleza kuwa kuimarika kwa mawasiliano kati ya nchi hizo tatu kunachangia utulivu, usalama wa upatikanaji wa nishati, na ustahimilivu wa kiuchumi kutoka Ulaya hadi Asia.
Kwa mujibu wa Fidan, kuongezeka kwa umuhimu wa Njia ya Kati (Middle Corridor) ndio ishara iliyo wazi zaidi ya lengo hilo.
Pia alitaja sherehe ya Juni 2 iliyohusiana na sehemu ya Georgia ya reli ya Baku-Tbilisi-Kars kufikia uwezo kamili wa kufanya kazi kama hatua muhimu, akisema kuwa kuongeza manufaa ya njia hiyo kutaleta thamani zaidi kwa eneo hilo.
Mchakato wa amani kati ya Azerbaijan na Armenia
Fidan alisema mawaziri hao watatu walithibitisha tena uelewa wa pamoja kwamba utulivu, amani na ustawi katika Caucasus Kusini vinapaswa kujengwa kupitia ushirikiano wa kweli na wenye kujenga.
Amesema kwamba, “Tunataka eneo letu lijulikane kwa miradi ya maendeleo badala ya migogoro, na kwa miradi ya ustawi wa pamoja na uunganishaji badala ya mgawanyiko.”
Ameeleza kuwa mchakato unaoendelea wa amani kati ya Azerbaijan na Armenia ndio mfano wenye matumaini zaidi wa dira hiyo.
“Tunaunga mkono mchakato wa amani kati ya Azerbaijan na Armenia. Pia tunatumaini kuwa wasiwasi ulio halali wa Azerbaijan utashughulikiwa na kwamba makubaliano ya amani yatasainiwa bila kuchelewa,” Fidan alisema.
Ameongeza kuwa: “Kwa mtazamo wetu, fursa na lengo kuu katika eneo la Caucasus Kusini ni hili: kadri misingi ya amani inavyozidi kuimarika, miradi ya mawasiliano itatoa matokeo makubwa zaidi. Na kadri mawasiliano yanavyoimarika, misingi ya kijamii na kiuchumi ya amani itazidi kuimarika.”
Mazungumzo ya Iran na Marekani
Pamoja na maendeleo chanya katika eneo la Caucasus Kusini, Fidan alionya kuwa mazingira mapana ya usalama wa kikanda bado yanakabiliwa na hatari kubwa.
Amesema mawaziri walijadili mazungumzo yanayoendelea kati ya Iran na Marekani, na kusisitiza umuhimu wa kuzuia mzozo ambao unaweza kuipeleka eneo na dunia “ukingoni mwa janga.”
Ameongeza kuwa Uturuki inaendelea kuwasiliana na Marekani na Iran, huku ikishauriana kwa karibu na nchi za kikanda, na kwamba Uturuki itaendelea kuunga mkono diplomasia na mazungumzo katika kipindi hiki muhimu.
Usalama wa urambazaji katika Bahari Nyeusi unazidi kudorora
Akijibu maswali ya waandishi wa habari, Fidan alisema usalama wa baharini katika Bahari Nyeusi umekuwa ukizorota taratibu kadri vita vinavyoendelea kupanuka.
Amesema: “Matukio haya yaliyoelezwa kwenye swali hilo yameonyesha mara kwa mara jinsi wasiwasi wa Rais wetu Recep Tayyip Erdogan kuhusu usitishaji vita katika vita vya Urusi na Ukraine ulivyokuwa wa msingi tangu mwanzo.”
Ameongeza kuwa athari za vita zimeenea zaidi ya uwanja wa mapigano, akitaja silaha na risasi zilizoonekana katika nchi za Baltiki kama Estonia, Lithuania na Latvia, pamoja na Romania.
Amesema mabomu ya baharini na vifaa vya kijeshi visivyo na rubani vimefika hadi maeneo ya Mlango wa Bahari wa Uturuki, na kwamba Georgia pia imeathiriwa na mashambulizi.
Ameeleza kuwa, “Kadri vita vinavyoendelea, tunaona jinsi vinavyoenea kijiografia. Pande husika sasa zinajaribu kulenga maeneo mapana zaidi ili kubadilisha uwiano wa kijeshi uliopo.”
Ameongeza kuwa takriban sasa hakuna tena mipaka kuhusu kulenga miundombinu au majengo ya juu, akisema hili linaonyesha ukubwa wa uharibifu wa vita.
Wasiwasi kuhusu usafiri wa raia baharini
Fidan aliashiria nafasi ya Uturuki katika kuwezesha Mpango wa Nafaka wa Bahari Nyeusi na kuuona kama mafanikio ya kihistoria.
Amesema: “Vivyo hivyo, kupungua kwa usalama wa urambazaji katika Bahari Nyeusi kutokana na kuongezeka kwa vita kunatuhangaisha sote.”
Ameongeza kuwa umuhimu wa kuhakikisha meli za kiraia za Uturuki na nchi nyingine hazilengwi, akionya kuwa ndege zisizo na rubani, makombora na makosa ya utambuzi katika maeneo ya vita vinaweza kusababisha majanga zaidi.
Mfano wa ushirikiano wa kikanda kwa maeneo mengine
Fidan amesema Uturuki inaona umiliki wa kikanda na ushirikiano kama nyenzo muhimu za kufanikisha utulivu na maendeleo, na akapendekeza kuwa mfano wa ushirikiano wa pande tatu na Azerbaijan na Georgia unaweza kutumika pia sehemu nyingine.
Amesema mifumo kama hiyo inapaswa kuendelezwa katika eneo la Balkan na Mashariki ya Kati ili kukuza amani na utulivu.
Fidan amesema, “Lengo letu ni kuanzisha ushirikiano wa kikanda na amani katika mabonde yote ya kimkakati ambako tupo, kuzuia migogoro au kupunguza ukali wake pale inapowezekana, na kuunda mazingira yanayowezesha maendeleo, ustawi, uhuru na haki za binadamu.”



















