Takriban Waislamu milioni 2 wanatarajiwa kutekeleza ibada ya Hajj huku mahujaji wakielekea Mina
ULIMWENGU
5 dk kusoma
Takriban Waislamu milioni 2 wanatarajiwa kutekeleza ibada ya Hajj huku mahujaji wakielekea MinaMahujaji wanaowasili Mina siku ya Jumatatu wataadhimisha Siku ya Tarwiyah, ambayo ni hatua ya kwanza ya hija ndani ya maeneo matakatifu na mwanzo rasmi wa ibada za Hajj.
Mahujaji wazuru Kaaba kabla ya Hajj ya kila mwaka, huko Makka. / / Reuters

Mapema alfajiri ya Jumatatu, mahujaji walianza kuelekea katika eneo takatifu la Mina magharibi mwa mji wa Makka, jambo lililoashiria mwanzo wa safari inayochukuliwa kuwa ya kiroho zaidi kwa Waislamu duniani kote.

Takriban Waislamu milioni 2 wanatarajiwa kutekeleza ibada ya Hajj mwaka 2026 huku Saudi Arabia ikiendelea kurekodi ongezeko la idadi ya mahujaji wanaowasili na kuimarisha maandalizi kwa msimu wa kila mwaka wa Hajj.

Mahujaji wanaowasili Mina siku ya Jumatatu wataadhimisha Siku ya Tarwiyah, hatua ya kwanza ya Hajj katika maeneo matakatifu na mwanzo rasmi wa ibada hio.

Kwa mujibu wa mapokeo, jina la Siku ya Tarwiyah linatokana na wazo kwamba mahujaji “wanajijaza” kiroho kwa imani na uchamungu wakijiandaa kwa kusimama Arafat, ambayo ndiyo ibada muhimu zaidi ya Hajj na hufanyika siku ya tisa ya Dhul-Hijjah, ambayo mwaka huu inaangukia Jumanne.

Katika Siku ya Tarwiyah, mahujaji hutumia muda wao katika dua, dhikri na tafakuri huku wakisoma dua ya Talbiyah.

Mahujaji pia huswali sala tano za kila siku wakiwa Mina kwa kupunguza rakaa bila kuziunganisha, na hulala huko kabla ya kuelekea Arafat baada ya jua kuchomoza siku ya tisa ya Dhul-Hijjah.

Umuhimu wa Mina katika dini

Mina haitumiki tu kama mwanzo wa ibada za Tarwiyah, bali pia ni mahali ambapo mahujaji hurudi katika Siku ya Kuchinja — siku ya kwanza ya Eid al-Adha, ambayo mwaka huu inaangukia Jumatano na huhusisha kuchinja wanyama kwa ajili ya ibada — pamoja na siku za Tashreeq, ambazo ni siku tatu baada ya Eid.

Mina ipo kati ya Makka na Muzdalifah, takriban kilomita 7 kaskazini mashariki mwa Msikiti Mkuu wa Makka, na ina ukubwa wa takriban kilomita za mraba 16.8 ndani ya mipaka yake ya kidini.

Eneo hilo ni bonde lililozungukwa na milima upande wa kaskazini na kusini, na hukaliwa tu wakati wa msimu wa Hajj.

Kwa mujibu wa wanahistoria, jina Mina linatokana na mzizi wa Kiarabu unaomaanisha “kumwaga damu,” kutokana na idadi kubwa ya wanyama wa dhabihu waliokuwa wakichinjwa hapo jadi.

Maelezo mengine yaliyotajwa katika kitabu Atlas of Hajj and Umrah: History and Jurisprudence yanaeleza kuwa eneo hilo liliitwa Mina kwa sababu Nabii Adam aliitamani Pepo hapo, au kwa sababu lilikuwa mahali pa watu kukusanyika, kulingana na taarifa ya Shirika la Habari la Saudi Arabia.

Mina pia ina umuhimu mkubwa wa kidini kwa sababu inahusishwa na Nabii Ibrahim, ambaye aliamrishwa kumtoa mwanawe dhabihu kabla ya kupewa kondoo kama mbadala kwa amri ya Mwenyezi Mungu.

Eneo hilo pia linajulikana kwa alama kadhaa muhimu za Hajj, ikiwemo nguzo tatu zinazotumika katika ibada ya kurusha mawe kwa shetani: Jamrat al-Aqaba tarehe 10 Dhul-Hijjah, pamoja na ibada za Jamarat katika siku za Tashreeq tarehe 11, 12 na 13.

Mina pia ina Msikiti wa Al-Khaif, ambako Mtume Muhammad alitoa Hotuba yake ya Kuaga.

Kihistoria, Mina pia ilishuhudia matukio muhimu katika historia ya mwanzo wa Uislamu, ikiwemo Ahadi ya Kwanza na ya Pili ya Aqaba katika mwaka wa 12 na 13 baada ya Hijra, wakati makundi ya Ansar walipompa Mtume Muhammad kiapo cha utiifu.

Miundombinu iliyopanuliwa na hatua za kukabiliana na hali ya hewa

Msemaji wa Wizara ya Hajj na Umra ya Saudi Arabia, Ghassan Al-Nuwaimi, alisema Jumapili jioni kuwa zaidi ya miradi 25 ya maendeleo imetekelezwa katika maeneo matakatifu, ikiwa ni ongezeko la asilimia 100 ikilinganishwa na mwaka uliopita.

“Miradi hiyo ilijumuisha kuongeza ukubwa wa Mina, kuandaa zaidi ya mahema 54,000, na kupanua mpango wa Green Holy Sites kwa kupanda zaidi ya miti 60,000,” alisema.

Mpango wa Green Holy Sites, ulioanzishwa mwaka 2025, unalenga kuongeza maeneo ya kijani na mimea katika maeneo matakatifu ili kuboresha ubora wa hewa na kuimarisha mazingira kwa mahujaji.

Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Saudi Arabia, kupandwa kwa zaidi ya miti 60,000 kutafanya maeneo ya kijani kuongezeka mara tatu katika maeneo matakatifu.

Shirika hilo pia liliripoti kuwa maeneo kadhaa yaliyokuwa hayatumiwi vizuri hapo awali yamebadilishwa kuwa maeneo ya matumizi kamili, jambo lililoongeza uwezo wa maeneo yaliyoboreshwa kufikia mahujaji takriban 209,000 katika misimu mitatu mfululizo ya Hajj, huku ongezeko la kila mwaka likiwa karibu mahujaji 70,000.

Shirika hilo liliongeza kuwa mahujaji wapatao 87,000 watanufaika na miradi ya kupanua eneo hilo katika msimu huu wa Hajj.

Wizara ya Hajj na Umra ya Saudi Arabia ilitangaza Jumapili kuwa maandalizi ya Siku ya Tarwiyah yamekamilika, huku mifumo ya uendeshaji na ya ardhini ikiwa tayari kwa usafirishaji wa mahujaji kuelekea Mina.

Mamlaka zilisema mfumo huo wa pamoja unajumuisha kusimamia harakati za mahujaji kuelekea mahema, kufuatilia ubora wa huduma, na kuratibu shughuli na taasisi husika.

Wizara hiyo ilisema kazi zake pia zinajumuisha kufuatilia usafiri wa mahujaji kutoka maeneo ya malazi kwenda Mina, kurahisisha kuingia kambini, kutoa huduma za mwongozo na elimu, na kuwasaidia mahujaji kufika katika maeneo yaliyotengwa kwa mujibu wa mipango rasmi ya uendeshaji.

Kwa upande mwingine, Kituo cha Kitaifa cha Hali ya Hewa cha Saudi Arabia kilitangaza utayari wake kwa Siku ya Tarwiyah, ikiwemo huduma za kutoa tahadhari za hali ya hewa kwa lugha tano kwa mahujaji na wafanyakazi.

Kituo hicho kilitabiri kuwa joto huko Mina litafikia nyuzi joto 45 Fahrenheit na kushuka hadi nyuzi joto 27 wakati wa Siku ya Tarwiyah, huku upepo wa kaskazini-magharibi hadi kaskazini ukifikia kilomita 35 kwa saa, kiwango cha unyevunyevu kikifikia asilimia 50, pamoja na hali ya mawingu kiasi na dhoruba za vumbi mara kwa mara.

CHANZO:AA