Kocha wa Cabo Verde Pedro Leitão Brito almaarufu Bubista aliingia katika mkutano wake na waandishi wa habari akiwa amejifunika bendera ya nchi yake, mtu wa maneno machache aliyepewa jukumu la kueleza jinsi moja ya mataifa madogo zaidi katika kandanda yalivyojitosa katika raundi ya mtoano ya Kombe la Dunia katika jaribio la kwanza.
Sare yao ya 0-0 na Saudi Arabia ilikamilisha safari ya hatua ya makundi ya sare tatu ambazo ziliwafanya kuambulia pointi tatu, wakitegemea kwa hofu Uhispania kuwalaza Uruguay ili wafuzu.
Kwa hivyo, wachezaji walibaki uwanjani wakiwa na simu mkononi, wakitazama dakika za mwisho za ushindi wa 1-0 wa Uhispania kabla ya kulipuka kwa vifijo za kushangilia.
Kwa Bubista, hata hivyo, hii haikuwa hadithi, lakini mafanikio yaliyojengwa juu ya bidii, nidhamu na kukataa kufifia chini ya shinikizo.
"Ninajivunia walichofanikisha," beki huyo wa zamani mwenye umri wa miaka 56 alisema. "Ili kumaliza awamu ya kwanza bila kupoteza mechi hata moja, lazima tufurahi, ilikuwa chini ya mpangilio na moyo wa timu.
"Mashabiki wetu wanastahili haya yote. Tulipungukiwa na bao moja kuwa bora zaidi, kuwa na furaha zaidi. Timu ilifanya kila walichoweza kushinda na nimefurahishwa."
Cabo Verde, taifa dogo zaidi kuwahi kufika hatua ya mtoano ya Kombe la Dunia, lilimaliza katika nafasi ya pili katika Kundi H, na kuwafanya wafuzu kwa raundi ya 32 na mabingwa Argentina, tuzo ambayo ilionekana kutowezekana hata ilipodhihirika wazi.
"Umoja na uvumilivu"
"Inashangaza kidogo, ingawa tulikuwa tukikumbuka kuwa tunaweza kufikia hatua hii baada ya mechi mbili za kwanza," alisema.
"Timu ilikuwa na nia ya kuonyesha ulimwengu wote kile tulichoumbwa nacho; tulijivunia kile ambacho tayari tumefanikiwa. Sisi ni nchi ndogo, lakini tunapigania kile tunachotaka kufikia. Kwetu, hakuna kisichowezekana."
Cabo Verde walikuwa na wasiwasi walipokuwa wakingojea habari kutoka kwa mechi ya Uhispania v Uruguay, lakini kocha wao alisema masaibu hayo yalifichua kiini halisi cha kikosi chake.
"Muhimu? Umoja wa timu yetu na uimara," alisema.
"Siku zote tumekuwa tukizungumza kuhusu utangamano wetu, lakini pia juu ya dhamira yetu ya kufanya mambo bila woga. Ilikuwa mechi ngumu sana iliyohitaji nguvu kubwa ya kiakili, kwani tulikuwa tunategemea matokeo ya mechi nyingine, lakini timu yetu ilionyesha tabia ya ajabu."
Bubista alisema wachezaji wake wanastahili kusifiwa si tu kwa soka lao bali kwa namna walivyovuka hatua ya makundi.
"Juhudi humpa mtu heshima," Bubista alisema. "Wachezaji wote walielewa umuhimu wa kazi ya kila siku.
Kukabiliana na Messi uwanjani
"Tuliwaambia wachezaji wanapaswa kufanya kazi kwa bidii na kujiamini kwa sababu malipo yatakuja. Na ndio hapa tulipo. Watu wa Cabo Verde wanapaswa kujivunia kile ambacho timu hii imefanya hadi sasa. Ni kitu cha ajabu."
Akitazamia kukutana na Argentina inayonolewa na Lionel Messi, Bubista aliandaa pambano hilo kama la heshima.
"Ni nchi ambayo tuna uhusiano wa muda mrefu, kwani watu wengi wa Cabo Verde wamehamia huko," alisema.
"Tutacheza mchezo wetu kwa mtazamo sahihi na hisia ya uwajibikaji, lakini pia kwa utu na tabia zetu wenyewe.
Wana Messi, ambaye hahitaji kutambulishwa.
"Tunawakilisha kisiwa chetu, lakini pia tunaiwakilisha Afrika. Ni fahari kubwa. Moja ya malengo yetu ilikuwa ni kuonesha ubora wa soka letu na nchi yetu. Hii inaonyesha kuwa hata nchi ndogo zinaweza kuthibitisha kuwa hakuna kinachoshindikana ukiwa na nguvu, dhamira, umakini, utashi na ustahimilivu."











