| Swahili
AFRIKA
2 dk kusoma
Tume ya Rais kuhusu ghasia za baada ya uchaguzi Tanzania yaongezewa siku 42 kuhitimisha uchunguzi
Muda huo wa nyongeza unalenga kuiruhusu tume hiyo kukamilisha ukusanyaji na uchambuzi wa ushahidi unaohusishwa na fujo zilizozuka katika maeneo kadhaa ya nchi wakati na baada ya upigaji kura.
Tume ya Rais kuhusu ghasia za baada ya uchaguzi Tanzania yaongezewa siku 42 kuhitimisha uchunguzi
Jaji Mkuu mstaafu Mohamed Chande Othman aliteuliwa kuchunguza sababu, mazingira na athari za ghasia za uchaguzi wa Okt 29 2025 Tanzania / Others
tokea masaa 9


Tanzania imeiongezea muda wa siku 42 tume ya uchunguzi ya rais inayochunguza vurugu na machafuko yaliyotokea baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, wakati timu hiyo ikikimbia kuhitimisha vikao na kuandaa ripoti yake ya mwisho.

Muda huo wa nyongeza unalenga kuiruhusu tume hiyo kukamilisha ukusanyaji na uchambuzi wa ushahidi unaohusishwa na fujo zilizozuka katika maeneo kadhaa ya nchi wakati na baada ya upigaji kura.

Rais Samia Suluhu Hassan aliunda tume huru mnamo Novemba 2025 chini ya Sheria ya Tume za Uchunguzi, kufuatia shinikizo la ndani na nje ya nchi kutaka uchunguzi wa kuaminika kuhusu mauaji, kukamatwa na madai ya ukiukaji wa haki za binadamu kuhusiana na kipindi cha uchaguzi.

Hatua hiyo ilikuja baada ya maandamano kuzuka siku ya uchaguzi na siku zilizofuata, yakichochewa zaidi na kutengwa kwa wagombea wakuu wa upinzani, ushindi wa kishindo wa chama tawala cha zaidi ya asilimia 97, na madai ya ukiukwaji mkubwa wa sheria.

Maundi ya waangalizi wa kikanda na kimataifa - ikiwa ni pamoja na Umoja wa Afrika na SADC - zilisema kura hiyo ilipungukiwa na viwango vya kidemokrasia, ikitaja vikwazo kwa shughuli za upinzani, usumbufu wa upigaji kura katika baadhi ya maeneo na uwazi mdogo katika mchakato wa kujumlisha kura.

Machafuko hayo yalisababisha mamia kukamatwa na vifo vingi, huku mashirika ya kutetea haki za binadamu na Umoja wa Mataifa yakitaka uchunguzi wa haraka, huru na wa uwazi kuhakikisha uwajibikaji na maridhiano ya kitaifa.

Tume hiyo ambayo inaongozwa na Jaji Mkuu mstaafu Mohamed Chande Othman ina jukumu la kuchunguza sababu, mazingira na athari za uvunjifu wa amani unaohusishwa na kipindi cha uchaguzi, inapendekeza uwezekano wa kulipwa fidia na mageuzi ya kitaasisi ili kuzuia kutokea tena kwa machafuko kama hayo.

Tume hiyo ambayo awali ilikuwa imepewa siku 90 kuhitimisha kazi yake imekuwa ikifanya mikutano ya hadhara na kukutana na maafisa wakuu serikalini, akiwemo Mwanasheria Mkuu wa Serikali, ikiwa ni sehemu ya hatua yake ya kukusanya ushahidi.

Kazi yake pia imechunguzwa baada ya vizuizi kuwekwa kwenye utangazaji wa vyombo vya habari vya baadhi ya vikao vya mashahidi, hatua ambayo wakosoaji wanasema inaweka mipaka ya uwazi na kuongeza shaka ya umma katika mchakato huo.

CHANZO:TRT Afrika Swahili