| Swahili
UTURUKI
2 dk kusoma
Israel yaishambulia Gaza na Ukingo wa Magharibi licha ya makubaliano ya kusitisha vita: Erdogan
Rais wa Uturuki Erdogan anasisitiza kuwa serikali ya Israel imeongeza mashambulizi yake, huku Waislamu wakiadhimisha mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Israel yaishambulia Gaza na Ukingo wa Magharibi licha ya makubaliano ya kusitisha vita: Erdogan
Erdogan alisema kuwa vikwazo vikubwa vya kuzuia kuingia kwa misaada ya kibinadamu Gaza vinaendelea. / / AA
tokea masaa 3

Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan amesema kuwa Israel imeendelea kuongeza mashambulizi yake dhidi ya Ukanda wa Gaza na Ukingo wa Magharibi unaokaliwa, licha ya kuwepo kwa makubaliano ya kusitisha mapigano.

“Licha ya usitishaji mapigano wa Oktoba 10 (2025), uliofanikishwa kupitia juhudi za Uturuki, serikali ya Israel, ambayo inapuuza sheria za kimataifa, inaendelea kuongeza mashambulizi yake dhidi ya Gaza na Ukingo wa Magharibi,” Erdogan alisema siku ya Jumatano wakati wa chakula cha futari jijini Ankara katika mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Alisema Wapalestina wa Gaza, wanaofunga saumu na kufuturu katika makazi ya muda yaliyojaa alama za risasi na vipande vya mabomu, katikati ya magofu huku wakikataa “kukubali ukandamizaji ”, wanaweka mfano mzuri wa imani kwa Waislamu.

Erdogan aliongeza kuwa bado kuna vikwazo vikubwa vinavyozuia kuingizwa kwa misaada ya kibinadamu katika eneo hilo.

“Vizuizi, ukiukwaji, na vitendo vya kiholela vya Israel katika kivuko cha mpaka cha Rafah, ambacho ni tegemeo kuu la Gaza, kwa bahati mbaya vinaendelea,” alisema.

Mshikamano na Palestina

Kiongozi huyo wa Uturuki pia alieleza matumaini kwamba siku hizi takatifu zitaleta nafuu na amani kwa watu wanaodhulumiwa duniani kote, “hasa watoto mashujaa wote wa Palestina”, na kusema kuwa dua na mshikamano wa Uturuki uko pamoja nao.

Israel ilianzisha mashambulizi makali dhidi ya Gaza Oktoba 8, 2023, na kuua zaidi ya watu 72,000, wengi wao wakiwa wanawake na watoto, na kujeruhi zaidi ya 171,000 wengine.

Usitishaji mapigano unaoungwa mkono na Marekani umeanza kutekelezwa Gaza tangu Oktoba 10.

Licha ya makubaliano hayo, vikosi vya Israel vimeripotiwa kufanya mamia ya ukiukwaji kupitia mashambulizi ya makombora na risasi, na kuua angalau watu 615 pamoja na kujeruhi zaidi ya 1,600 wengine, kwa mujibu wa mamlaka za afya za Gaza.

CHANZO:AA