Tafrani baada ya kurushwa bomu la moshi alipo Waziri Mkuu wa Japan Fumio Kishida

Tafrani baada ya kurushwa bomu la moshi alipo Waziri Mkuu wa Japan Fumio Kishida

Taarifa zinasema Waziri Mkuu wa Japani hakujeruhiwa baada ya mlipuko wakati wa hafla ya kampeni
Mwanamume anayeaminika kuwa mshukiwa aliyerusha kitu kinachofanana na bomba karibu na Waziri Mkuu wa Japan Fumio Kishida wakati wa hotuba yake ya nje, anashikiliwa na maafisa wa polisi. Wakayama / Photo: Reuters

Waziri Mkuu wa Japan Fumio Kishida aliondolewa bila kujeruhiwa mapema Jumamosi baada ya mtu kurusha kilipuzi kuelekea upande wake alipokuwa akifanya kampeni katika bandari ya wavuvi magharibi mwa Japan, maafisa walisema.

Mpaka sasa taarifa zinasema hakuna aliyeumia, Kishida alipanga kuendelea na kampeni zake Jumamosi.

Eneo hilo la machafuko lilikumbusha mauaji ya Waziri Mkuu wa zamani Shinzo Abe, miezi tisa iliyopita, ambapo pia alikuwa amekuja kwenye ziara ya kampeni

Kishida alikuwa akitembelea bandari ya Saikazaki katika mkoa wa Wakayama ili kumuunga mkono mgombeaji wa chama tawala katika uchaguzi wa eneo hilo, na mlipuko huo ulitokea kabla tu ya kuanza hotuba yake, limeandika shirika la habari la AP

Kijana anayeaminika kuwa mshukiwa alikamatwa hapohapo katika eneo la tukio baada ya kudaiwa kurusha "kitu kinachotiliwa shaka," Katibu Mkuu wa Baraza la Mawaziri Hirokazu Matsuno aliwaambia waandishi wa habari.

Matsuno alikataa kuzungumzia nia na historia ya mshukiwa, akisema polisi bado wanachunguza.

Picha za runinga zinamuonyesha Kishida akiwa amesimama na kuupa mgongo umati wa watu.

Timu yake ya usalama ghafla inaelekea chini karibu naye, na waziri mkuu anazunguka huku na huko, akionekana kuwa na wasiwasi.

Kamera inageukia umati upesi wakati watu kadhaa, wakiwemo polisi waliovalia sare na waliovalia kiraia, wanakutana na kijana aliyevalia barakoa nyeupe ya upasuaji na kushikilia kile kinachoonekana kuwa kifaa kingine, bomba refu lenye rangi ya sarafu.

AP