Malalamiko ya Ulaya yaongezeka juu ya vita vya Israel vya Gaza, huku maandamano yakiendelea

Malalamiko ya Ulaya yaongezeka juu ya vita vya Israel vya Gaza, huku maandamano yakiendelea

Maelfu ya waandamanaji wanakusanyika katika mitaa ya miji mikubwa ya Ulaya kwa mshikamano na Wapalestina.
Maandamano ya kutaka kusitishwa kwa mapigano huko Gaza yanafanyika mjini Barcelona. / Picha: Reuters

Watu kote barani Ulaya wameendelea kumiminika mabarabarani kueleza mshikamano wao na Palestina na kulaani mashambulizi yanayoendelea ya Israel dhidi ya Gaza.

Kwa ujasiri, wakistahamili hali ya hewa ya mvua, watu wapatao 2,000 walikusanyika mjini Amsterdam siku ya Jumamosi, wakiwa wamebeba bendera za Palestina na kuimba nyimbo za kutia moyo "Kutoka mtoni hadi baharini, Palestina itakuwa huru," "Sitisha mapigano sasa," na "Komesha mauaji ya kimbari huko Palestina."

Mmoja wa washiriki Cillia Ferrier alishikilia kuwa kilichokuwa kikifanyika Palestina ni ubaguzi wa rangi, huku muandamanaji mwingine, Bart, akiitaka serikali ya Uholanzi kuikomesha Israel.

Nchini Poland, mamia ya watu waliandamana katika mji mkuu wa Warsaw katika mshikamano na Wapalestina huko Gaza wakiwa na mabango yanayosisitiza juu ya mauaji ya watoto na raia yanayofanywa na Israel.

Wakati huo huo, maandamano ya ushiriki mkubwa yaliandaliwa katika mji mkuu wa Austria Vienna ili kumaliza uvamizi wa Israel wa Gaza.

Mwanaharakati Medina Altagic alisema kuwa alikuwa hapa kuonyesha uungaji mkono wake kwa Wapalestina huko Gaza, ambao alisema wameuawa kwa wiki kadhaa, na akahimiza mshikamano wa umma nao.

Nchini Ujerumani, mamia ya watu walifanya maandamano ya kuunga mkono Palestina mjini Berlin.

Jakub Bielecki, ambaye alishiriki katika maandamano hayo, alisema: "Niko hapa kuonyesha mshikamano na watu wa Palestina wanaoshambuliwa kwa mabomu na wanajeshi wa Israeli, na kwa bahati mbaya, kusema wazi dhidi ya uungaji mkono usioyumba kwa Israeli huko Ujerumani kunazuiwa.

"Hili haliulizwi, na inanifanya nikose raha. Watoto wanakufa, na inanifanya nikose usingizi. Niko hapa kusema hauko peke yako."

Kundi la madaktari waliandamana wakiwa wameziba midomo kuashiria shambulio la mabomu katika hospitali za Gaza na mauaji ya raia.

Maelfu pia walikusanyika katika uwanja wa Parc Des Cropettes huko Geneva, Uswisi, kupinga mashambulizi ya Israel dhidi ya Gaza.

Licha ya baridi kali, waandamanaji waliandamana hadi Ofisi ya Umoja wa Mataifa mjini humo.

TRT World