Ukame huo umesababisha hekta za mazao ya mahindi kuharibiwa. Picha / Reuters

Zambia inapanga kuagiza tani 650,000 za mahindi meupe kutoka Tanzania baada ya ukame kupunguza uzalishaji kwa zaidi ya asilimia 50%, Waziri wa Habari Cornelius Mweetwa alisema Jumatano.

Uzalishaji wa mahindi wa Zambia katika msimu wa mazao wa 2023/2024 unatarajiwa kupungua hadi tani milioni 1.5 kutoka tani milioni 3.2 msimu uliopita, kulingana na uchunguzi wa utabiri wa mazao.

"Serikali imefikia makubaliano ya awali na serikali ya Tanzania kuagiza tani 650,000 za mahindi meupe," Mweetwa alisema katika taarifa akitangaza maamuzi ya baraza la mawaziri.

Ukame mbaya

Mnamo Aprili, Rais Hakainde Hichilema alisema nchi inahitaji karibu dola bilioni 1 kukabiliana na ukame mbaya zaidi ambao nchi imewahi kupata.

Alisema karibu nusu ya watu milioni 20 nchini wameathiriwa vibaya na kipindi kirefu cha ukame kilichosababishwa na hali ya hewa ya El Nino.

Waziri wa Kilimo Mtolo Phiri alisema bungeni Jumanne kuwa nchi imesitisha usafirishaji wa mahindi nje ya nchi kufuatia upungufu wa tani milioni 2.1 na itaagiza nafaka hiyo muhimu.

Zambia ilitangaza ukame kuwa janga la kitaifa mnamo Februari ambapo zaidi ya watu milioni 6 walikuwa wanahitaji msaada wa haraka wa kibinadamu.

TRT Afrika na mashirika ya habari