Mmarekani Tyler Thompson Jr, katikati, ameketi kortini mjini Kinshasa, Ijumaa, Juni 7, 2024. / Picha: AP

Mahakama ya kijeshi katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) imetoa hukumu ya kifo kwa watu 37 wakiwemo Wamarekani watatu baada ya kuwatia hatiani kwa tuhuma za kushiriki katika jaribio la mapinduzi.

"Mahakama inatangaza hukumu kali zaidi: adhabu ya kifo," rais wa mahakama Freddy Ehume alisema siku ya Ijumaa, kufuatia kesi ya watu 51 iliyoanza mapema Juni.

Washtakiwa, ambao pia ni pamoja na Muingereza, Mbelgiji, Canada na Wakongomani kadhaa, wanaweza kukata rufaa dhidi ya hukumu hiyo kwa tuhuma zinazojumuisha ugaidi, mauaji na chama cha uhalifu. Watu kumi na wanne waliachiliwa huru katika kesi hiyo.

Watu sita waliuawa wakati wa jaribio la mapinduzi lililoshindwa lililoongozwa na kiongozi wa upinzani Christian Malanga mwezi Mei ambalo lililenga ikulu ya rais na mshirika wa karibu wa Rais Felix Tshisekedi. Malanga aliuawa kwa kupigwa risasi akipinga kukamatwa mara tu baada ya kutiririsha moja kwa moja shambulio hilo kwenye mtandao wake wa kijamii, jeshi la Congo lilisema.

Mtoto wa kiume wa Malanga, Marcel Malanga, mwenye umri wa miaka 21, ambaye ni raia wa Marekani, na Wamarekani wengine wawili walipatikana na hatia katika shambulio hilo. Mama yake, Brittney Sawyer, amesema mwanawe hana hatia na alikuwa akimfuata tu baba yake, ambaye alijiona kuwa rais wa serikali butu uhamishoni.

Wamarekani wengine walikuwa Tyler Thompson Jr, ambaye alisafiri kwa ndege hadi Afrika kutoka Utah na Malanga mdogo kwa kile familia yake iliamini kuwa likizo, na Benjamin Reuben Zalman-Polun, 36, ambaye anaripotiwa kumfahamu Christian Malanga kupitia kampuni ya kuchimba dhahabu.

Kampuni hiyo ilianzishwa nchini Msumbiji mwaka 2022, kulingana na jarida rasmi lililochapishwa na serikali ya Msumbiji, na ripoti ya jarida la Ujasusi la Afrika.

Familia ya Thompson inashikilia kuwa hakuwa na ufahamu wa nia ya mzee Malanga, hana mpango wa harakati za kisiasa na hakuwa na mpango hata wa kuingia DRC. Yeye na akina Malanga walikusudiwa kusafiri tu hadi Afrika Kusini na Eswatini, mama wa kambo wa Thompson alisema.

Kusomwa kwa hukumu na hukumu mbele ya mahakama ya wazi ya kijeshi ilitangazwa moja kwa moja kwenye televisheni.

Mwezi uliopita, mwendesha mashtaka wa kijeshi, Lt Kanali Innocent Radjabu alitoa wito kwa majaji kuwahukumu kifo washtakiwa wote, isipokuwa mmoja ambaye ana matatizo ya kisaikolojia.

Mapema mwaka huu, DRC ilirejesha hukumu ya kifo, na kuondoa usitishaji uliodumu kwa zaidi ya miongo miwili, huku mamlaka ikipambana kuzuia ghasia na mashambulizi ya wanamgambo nchini humo.

TRT Afrika na mashirika ya habari