"Netanyahu na watu wenye msimamo mkali kama yeye ni wahusika wa uvamizi, mauaji ya kikabila, na uhalifu wa kivita," Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Türkiye Fahrettin Altun alisema. / Picha: AA

Kujibu maneno ya hivi majuzi kutoka kwa Waziri Mkuu wa Israeli Benjamin Netanyahu na Waziri wa Mambo ya Nje Eli Cohen, ambayo yalimlenga Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan, Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Uturuki Fahrettin Altun alikataa kwa dhati majaribio yao ya kugeuza mawazo kutoka kwa kile alichokiita "uhalifu wa kivita dhidi ya raia."

"Hatushangazwi na juhudi za Waziri Mkuu wa Israeli na Waziri wa Mambo ya Nje za kuwatenganisha na uhalifu wao wa kivita dhidi ya raia," Altun alisema Alhamisi.

Aliendelea kuangazia mtindo wa upotoshaji wa serikali ya Israeli kuhusu vitendo vyao huko Gaza, akisisitiza kuwa rais Erdoğan anasalia na nia ya kusema ukweli.

“Rais wetu Erdogan hajawahi kuogopa kusema ukweli na ataendelea kufanya hivyo,” alitangaza Altun.

Akisisitiza matukio yanayoonekana kwa uwazi huko Gaza katika kipindi cha mwezi mmoja uliopita, alisisitiza kwamba hakuna kiasi cha taarifa potofu kinachoweza kuficha ukweli unaoshuhudiwa na ulimwengu.

'Netanyahu anadhoofisha amani'

Akimtaja Waziri Mkuu wa Israeli Netanyahu moja kwa moja, Altun alimfafanua kama mtu ambaye ametumia miongo kadhaa kudhoofisha matarajio ya amani.

"Kama mwanasiasa ambaye alijenga taaluma yake katika kuharibu nafasi yoyote ya amani kwa miongo kadhaa, Netanyahu ni wazi hawezi kujishughulisha na kusikiliza ukweli kuhusu vita vyake visivyo na maana vinavyolenga raia wa Palestina," mwakilishi wa Uturuki alisema.

Akimtuhumu Netanyahu na washiriki wengine wenye msimamo mkali wa serikali ya Tel Aviv kushiriki katika uvamizi, mauaji ya kikabila, na uhalifu wa kivita, Mkurugenzi wa Mawasiliano alisisitiza kutokuwa na nia ya kudumisha amani katika eneo hilo. "Hawana nia ya kujenga amani katika eneo hili na wataendelea kusukuma vita kwa fursa yoyote watakayopata," alitangaza.

"Lazima dunia ichukue hatua sasa kuhakikisha amani ya kudumu ingawa wanasiasa wa Israeli wanasisitiza juu ya ghasia za kudumu," alihimiza Altun. Ametoa wito wa kuwepo umoja wa kimataifa katika kutafuta amani ya haki, akilaani jinai zinazofanywa na wanasiasa wa Israeli dhidi ya raia wa Palestina.

"Lazima tuungane kwa ajili ya amani ya haki " alisema Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Uturuki.

Alipuuzia mashambulizi dhidi ya uongozi wa Uturuki kuwa ni uongo na kashfa, akishikilia kuwa Israeli tayari ilikuwa imeshindwa katika mahakama ya maoni ya umma.

"Licha ya kampeni za kimfumo za uhamasishaji wa vita na upotoshaji wa Israeli, tunasalia kujitolea kufanya kila tuwezalo kwa ajili ya amani. Uturuki kamwe haitaiacha Palestina!" alihitimisha taarifa hiyo, akirejea uungaji mkono usioyumba wa Uturuki kwa Palestina.

Tangu Oktoba 7 2023, baada ya Israeli kuanza kushambulia kwa mabomu Gaza kufuatia shambulio la Hamas, Wapalestina wasiopungua 11,500 wameuawa, wakiwemo karibu wanawake na watoto 8,000, huku wengine zaidi ya 30,000 wamejeruhiwa, kulingana na takwimu za hivi punde kutoka kwa mamlaka ya Palestina.

TRT World