Netherlands Soccer Ajax Onana / Photo: AP

Kwa mujibu wa orodha fupi ya Kipa bora wa kiume wa tuzo ya FIFA 2023, golikipa wawili wa Afrika ni miongoni mwa wadakaji watano waliong'aa duniani ndani ya kipindi hicho.

Golikipa wa Cameroon, Andre Onana ambaye alijiunga na Manchester United mwezi Julai, alikuwa na mwaka wa kufaana kwa kutoa mojawapo ya maonyesho bora ya kipa wa mwaka hasa katika fainali ya Ligi ya Mabingwa ya 2023 jijini Istanbul, Uturuki.

Andre Onana Cameroon na Manchester United. Picha: FIFA

Onana alifanya msururu wa uokoaji maridadi na kuvutia kwa usambazaji wake wa mpira akicheza kama kiungo wa kati.

Hata licha ya timu yake ya awali ya Inter Milan kufungwa na Manchester City 1-0, alijiongezea sifa kama mmoja wa wachezaji mashuhuri wa ulimwengu langoni.

Yassine Bounou

Golikipa wa timu ya Morocco, Bounou, alidumisha fomu yake bora baada ya kuchangia pakubwa na kutekeleza majukumu muhimu kwenye safari ya kihistoria ya Morocco ya kutinga hadi nusu fainali ya Kombe la Dunia la FIFA 2022™ nchini Qatar.

Kabla ya kusainiwa na klabu ya Saudi Arabia ya Al-Hilal mnamo mwezi Agosti 2023, Bounou aliiwezesha Sevilla kuweka rekodi ya kujiongezea taji la saba la Ligi ya Europa ya UEFA.

Yassine Bounou alikuwa shujaa kwenye mikwaju ya penalti walipoishinda Roma katika fainali. Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 32, ni matumaini ya Morocco kwenye dimba la Afcon mwaka ujao Abidjan.

Kipa wa Morocco Yassine Bounou. Picha: FIFA

Bounou, na Onana wanatarajiwa kushuhudia ushindani mkali kutoka kwa:Thibaut Courtois wa Ubelgiji na Real Madrid, Ederson wa Brazil na Manchester City,

Ederson wa Man City Picha: Getty

na Ter Stegen wa Ujerumani na Barcelona.

TRT Afrika