JKT Queens kutoka Tanzania. Picha: CECAFA

Ingawa Buja Queens ya Burundi imenyakua nafasi ya tatu kwa kushinda 1-0 dhidi ya Vihiga Queens kutoka Kenya, mwakilishi wa Afrika Mashariki bado hajajulikana.

Malkia wa soka ya wanawake JKT Queens kutoka Tanzania wnapigiwa upatu kwenye fainali dhidi ya vipusa wa Benki ya Biashara ya Ethiopia wakisaka uwakilishi wa Kanda ya CECAFA kwenye Ligi ya Mabingwa CAF kwa Wanawake.

Licha ya kuwa kwenye kombe hilo kwa mara ya kwanza, JKT Queens wameonyesha ubabe wao kwenye ngarambe hizo wakisajili ushindi wa 100% baada ya kuwatesa AS Kigali Women, New Generation ya Zanzibar na Vihiga Queens kutoka Kenya katika hatua ya makundi na kuibandua Buja Queens kutoka Burundi kwenye hatua ya mtoano.

Hata hivyo, Kocha wa JKT Queens, Esther Fredy Chaburuma ambaye pia ni kocha msaidizi wa timu ya taifa ya wanawake, ameweka wazi kuwa fainali ni hatua tofauti na mechi za awlai licha ya kushinda mechi zote nne za mashindano hayo.

CBE FC ya Ethiopia. Picha: CECAFA

"Tunafuraha kufika fainali, lakini tunajua kuchuana na timu ya Ethiopia haitakuwa kazi rahisi. Tunahitaji kujiandaa vyema kwa sababu ninawaamini wachezaji wangu iwapo tutacheza kwa mpango," Esther alisema.

Aidha, timu ya wanawake kutoka Ethiopia, Benki ya Biashara ya Ethiopia, ambayo ilipoteza fainali za 2021 kwa Vihiga Queens, pia ndiyo timu iliyofunga mabao mengi zaidi kwenye shindano hili ikiwa na mabao 17. Waliishinda Vihiga Queens ya kenya, katika nusu fainali

"Haikuwa rahisi kufika fainali kwa sababu timu zote kwenye mashindano zimeimarika sana. Lakini sisi ni timu yenye uzoefu kuliko JKT Queens katika kiwango hiki na lazima tuonyeshe hilo kwenye fainali. Hatutazichukulia kawaida, lakini tunajua nini cha kutarajia na nini cha kufanya juu yake, "aliongeza Birhanu Gizaw Heye, kocha wa CBE FC ya Ethiopia.

Mshindi wa fainali hiyo atawakilisha Kanda ya CECAFA kwenye Ligi ya Mabingwa ya Wanawake ya CAF itakayofanyika baadaye mwaka huu nchini Cote d’Ivoire.

TRT Afrika