Mwanamuziki huyo alifariki akiwa na umri wa miaka 48./Picha: Getty Images

Mashabiki wa muziki duniani wamemkumbuka gwiji wa muziki duniani Whitney Houston, ambaye aliachia albamu yake ya ‘You Give Good Love’ siku kama ya leo, miaka 39 iliyopita.(February 22, 1985).

Whitney alikutwa na umauti, miaka 12 iliyopita katika hoteli ya Beverly Hills, kulingana na taarifa iliyotolewa na wachunguzi wa maiti.

Wimbo wake 'You Give Good Love’ ulimpa umaarufu kwani ndio kibao kilichompa Houston nafasi ya kuonekana kama mwimbaji wa kike mweusi baada ya kushika nafasi ya kwanza kwenye orodha ya Marekani ya Billboard Hot Black Singles.

Wimbo huo, pia ulichaguliwa kama kazi bora katika kipengele cha wimbo bora wa R&B katika tuzo za 28 za Grammy zilizofanyika mwaka 1986.

Whitney Houston ni mshindi wa tuzo 6 za Grammy./Picha: Getty Images.

Wasanii wengi wanamuelezea nyota huyo kama mmoja wa watu wenye ushawishi mkubwa kwenye tasnia ya muziki duniani.

‘’Mwanamuziki bora wa wakati wote, Lady Witney Houston’’ alisema shabiki , @medicboyc, kwenye ukurasa wa X.

Nyota huyo, pia anakumbukwa kwa kibao chake cha ‘’Greatest Love of All'', ambacho mwanzoni kilirekodiwa na George Benson, mwanamuziki mwingine kutoka Afrika, mwenye asili ya Afrika.

Baadhi ya maneno ya utangulizi kwenye tungo hiyo: I believe the children are our future. Teach them well and let them lead the way’’, yanaelezwa kuwa ujumbe mujarab, hasa kwa wakati huu ambapo watoto wengi wanapitia changamoto mbalimbali, ikiwemo vita na machafuko ya kisiasa duniani.

Whitney Houston amejizolea sifa kemkem kutokana na ujumbe unaotawala kwenye nyimbo zake./Picha:Getty Images

Whitney alitoa wimbo huo, maalumu kwa watoto duniani, akiamini kuwa ni wajibu wa watu wazima kufanya jitihada ya kuwaimarisha kufikia ujana wao. Pia anatumia wimbo huo, kuwambukusha watoto kuwa wao ndio taifa la baadae litakaloongoza dunia.

Mwaka jana, wanamuziki tajwa wakiwemo Ariana Grande, Beyonce, na Mariah Carey kutoka Marekani, walikiri kuendelea kuhamasika na nguvu ya jumbe kwenye tungo za Whitney Houston.

Kama kumbukumbu kwa nyota huyo, Ariana Grande aliimba baadhi ya nyimbo maarufu za Houston na kisha kuandika kwenye ukurasa wake X, “ni heshima kumuenzi malaika wangu usiku wa leo.”

Beyonce alisema, “Mara zote, nimetamani sana kuwa kama yeye. Alikuwa ni gwiji, mwanamke wa kipekee kabisa.”

Kutoka Afrika ya Kusini, pengine Belinda Davids ndiye alitoa wasifu wenye nguvu zaidi kwa Whitney kwa kuimba kwa sauti ya juu kabisa, kama alivyofanya Whitney mwenyewe.

TRT Afrika