Tingatinga likiendelea na zoezi la uokoaji katika eneo la tukio. /Picha: AFP

Watu nane, wakiwemo watoto wawili wamepoteza maisha kufuatia kuporomoka kwa dampo katika jiji la Kampala, nchini Uganda siku ya Jumamosi.

Vyombo vya habari nchini humo vinasema kuwa nyumba, watu na wanyama wameathirika na maporomoko ya udongo kwenye eneo la kutupa taka huko Kiteezi, wilaya ya kaskazini mwa Kampala, kufuatia kunyesha kwa mvua kubwa.

"Kwa masikitiko makubwa, hadi sasa watu nane, watu wazima sita na watoto wawili wamepatikana wamekufa katika eneo hilo," ilisema taarifa iliyochapishwa kwenye ukurasa wa X wa Mamlaka ya Jiji la Kampala (KCCA).

Mamlaka ya Jiji la Kampala inayoendesha eneo hilo la kutupia takataka, inasema kuwa watu 14 wameokolewa na kupelekwa hospitalini.

Uokoaji unaendelea

"Zoezi la uokozi linaendelea, tutaendelea kutoa taarifa muhimu kadiri tutakavyozipata," iliongeza taarifa hiyo.

Taswira za picha kutoka eneo la tukio lilionesha tingatinga likijaribu kuhamisha vifusi ili kupata manusura na miili mingine.

KCCA ilisema kulikuwa na "hitilafu ya kimuundo katika wingi wa taka asubuhi ya leo na kusababisha sehemu ya jaa kuporomoka".

Onyo la Afya

"Timu zetu, pamoja na mashirika mengine ya serikali yapo katika eneo la tukio kuchukua hatua zinazohitajika ili kuhakikisha eneo hilo liko salama na kuzuia matukio yoyote zaidi," iliongeza.

Gazeti la The Daily Monitor la nchini Uganda, lilisema kwenye tovuti yake kwamba mkuu wa mamlaka ya jiji hilo Erias Lukwago alionya mwezi Januari kwamba watu wanaofanya kazi na wanaoishi karibu na dampo la Kiteezi wako katika hatari nyingi za kiafya kutokana na kufurika kwa taka.

TRT Afrika