Vikosi vya usalama vya Somalia vyazuia shambulio la kujitoa mhanga katika kambi ya jeshi

Vikosi vya usalama vya Somalia vyazuia shambulio la kujitoa mhanga katika kambi ya jeshi

Mamlaka inasema mshukiwa wa kujitoa mhanga ameuawa Jumatatu asubuhi.
Vikosi vya usalama vya Somalia vimekuwa vikipambana na kundi la al-Shabaab kwa miaka mingi. Picha: AFP

Vikosi vya usalama nchini Somalia vimezuia jaribio la kujitoa muhanga katika kambi ya jeshi huko Mogadishu Jumatatu asubuhi, shirika la habari la serikali SONNA linaripoti.

Mshambulizi huyo aliuawa na wanajeshi wa Jeshi la Kitaifa kabla ya kulipua vilipuzi vyake, inaongeza.

Hakuna majeruhi wengine walioripotiwa kutokana na tukio hilo. Somalia imekuwa ikipambana na kundi la al-Shabaab kwa miaka mingi huku kundi hilo likifanya mashambulizi ya mara kwa mara ya kuua.

Wiki iliyopita, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa liliidhinisha kuahirishwa kuondoka kwa wanajeshi wa kulinda amani wa Umoja wa Afrika kutoka Somalia.

Kuchukua jukumu la usalama

Uamuzi huo unafuatia ombi la taifa hilo la Pembe ya Afrika la kutaka vikosi hivyo kusalia nchini humo kusaidia katika mapambano dhidi ya kundi la al-Shabab.

Ombi la Somalia liliungwa mkono na Umoja wa Afrika, nchi zote zinazochangia wanajeshi katika kikosi hicho na baraza, ambalo lilikubali kuchelewesha kuondoka kwa wanajeshi 19,000 wa AU kwa siku 90.

Mwaka jana mwezi Aprili, baraza hilo kwa kauli moja liliidhinisha Ujumbe mpya wa Mpito wa Umoja wa Afrika nchini Somalia, unaojulikana kama ATMIS, kusaidia Wasomali hadi majeshi yao yatakapowajibika kikamilifu kwa usalama wa nchi hiyo mwishoni mwa 2024.

ATMIS ilichukua nafasi ya misheni ya Umoja wa Afrika nchini Somalia, inayojulikana kama AMISOM, ambayo imekuwa katika taifa hilo la Pembe ya Afrika kwa miaka 15 kusaidia ujenzi wa amani nchini Somalia.

TRT Afrika